Rais Trump kuzungumza na Putin kwa simu leo Jumatatu
19 Mei 2025Rais wa Marekani Donald Trump anatazamiwa kuzungumza kwa njia ya simu na Rais wa Urusi Vladimir Putin leo hii Jumatatu kuhusu mipango ya usitishaji wa vita kati ya Urusi na Ukraine.
Trump ameandika katika mtandao wake wa kijamii wa Truth Social, kwamba anatumai mazungumzo yake na Putin yatafaulu kufikiwa makubaliano ya pande mbili ya kusitisha kwa vita.
Alipoingia madarakani katika muhula wake wa pili mapema mwaka huu, Trump aliahidi kwamba atahakikisha anavimaliza vita hivyo haraka iwezekanavyo lakini tangu wakati huo jitihada zake bado zinaonekana kutozaa matunda.
Wiki iliyopita, wawakilishi wa Urusi na Ukraine walifanya mazungumzo yao ya kwanza ya moja kwa moja ya amani huko Uturuki, baada ya miaka kadhaa ya kutofanikiwa kufikia makubaliano ya usitishaji mapigano.