Qatar: Kongo na M23 bado wamo kwenye mchakato wa amani
20 Agosti 2025Hayo yameelezwa Jumanne na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Qatar, Majed al-Ansari, wakati akizungumza na waandishi habari.
''Jambo zuri ni kwamba pande zote mbili zinajihusisha kikamilifu. Pia tunashirikiana nao kwa karibu sana, na tumejizatiti katika kuusimamia mchakato huu. Nadhani wahusika wameonyesha nia ya kukubaliana ambayo haikuwepo hapo awali,'' alifafanua al-Ansari.
Serikali ya Kongo na kundi la M23 walisaini makubaliano ya kusitisha mapigano mwezi Julai, yenye lengo la kukomesha kabisa vita ambavyo vimeligubika eneo la mashariki lenye utajiri mkubwa wa madini.
Kulingana na masharti ya mkataba huo, uliotokana na mazungumzo ya Qatar ambayo ni mpatanishi, pande hizo mbili zilipaswa kuanza mazungumzo ya amani Agosti 8 na kukamilisha makubaliano ifikapo Agosti 18.