Viongozi wa Ulaya waitisha mkutano wa dharura Paris
17 Februari 2025Mkutano huo unafanyika baada ya mkutano wa usalama wa mjini Münich kushindwa kukamilika vyema huku ukiwa umegubikwa na hali ya sintofahamu.
Viongozi kutoka Ujerumani, Uingereza, Italia, Poland, Uhispania, Uholanzi na Denmark wanatarajiwa kuhudhuria mkutano huo maalumu mjini Paris sambamba na Rais wa Baraza la Ulaya Antonio Costa, Rais wa Halmashauri kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO Mark Rutte.
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ameuitisha mkutano huo ili kuanzisha majadiliano kuhusu hali ya Ukraine pamoja na changamoto za usalama barani Ulaya.
Soma zaidi: Mkutano wa usalama mjini Munich waingia siku yake ya mwisho
Madhumuni ya mkutano huo ni kutafuta mkakati wa pamoja wa kushughulikia masuala kadhaa ambayo Ulaya haiwezi kuyakubali kwenye mchakato wa kutafuta amani na kuumaliza mzozo wa Ukraine.
Mataifa ya Ulaya na Ukraine yana hofu kuwa Marekani na Urusi zinaweza kufanya juhudi za kurejesha amani zenyewe bila kuzishirikisha nchi za Ulaya na Ukraine yenyewe baada ya Rais Donald Trumo kutangaza dhamira yake ya kuumaliza mgogoro huo na kuzungumza na Rais Vladimir Putin. Ras wa Ukraine Volodymyr Zelensky kwa upande wake amesema hatokubali uamuzi wowote unaoihusu Ukraine utakaofikiwa kati ya Trump na Putin.
Ulaya na Ukraine zinasisitiza kuwa zinapaswa kuwa sehemu ya mazungumzo hayo ya kutafuta amani. Kuhusu suala hilo Kansela wa Ujerumani anayewania pia kiti cha Ukansela katika Uchaguzi wa baadaye mwezi huu amesema ni lazima Ulaya ihusishwe kwani hakuna linalowezekana bila kuhusishwa viongozi wa bara hilo.
Mkutano wa Münich wafananishwa na "jinamizi" kwa Ulaya
Katika mkutano wa awali wa usalama uliofanyika mjini Münich nchini Ujerumani na kuhudhuriwa na viongozi wa dunia. Mkuu wa mkutano huo uliohitimishwa jana Jumapili Christoph Heusgen aliutaja kuwa ulikuwa mfano wa jinamizi kwa Ulaya licha ya kuwa umetoa mwanga zaidi.
Heusgen amesema kuwa maadiliano katika kushanyiko hilo yalionesha kuwa Marekani chini ya utawala wa Trump iko katika ulimwengu mwingine. Itakumbukwa kuwa Marekani imezitupia pialawama baadhi ya nchi za Umoja wa Ulaya kuwa zinakandamiza demokrasia na Uhuru wa habari
Maoni ya Heusgen yalitolewa muda mfupi baada ya Makamu wa Rais wa Marekani JD Vancekuwashambulia washirika wake wa Ulaya kwa kuhatarisha demokrasia kwa kuvitenga vyama vya kizalendo na kushindwa kutilia maanani masuala ya uhamiaji.
Heusgen wakati wa maoni ya kuhitimisha mkutano huo aliweka bayana shinikizo linaloikabili Ulaya kutokana misimamo ya Trump na kusema kuwa, ''Ni wazi kwamba utaratibu wetu wa Kimataifa unaozingatia sheria uko katika shinikizo kubwa. Ni imani yangu kubwa kuwa dunia hii inahitaji kuzingatia kanuni na misingi ya pamoja ya Umoja wa Mataifa na Azimio la Kimataifa la Haki za Binadamu. Utaratibu huu ni rahisi kuvurugwa na kuharibiwa lakini ni mgumu zaidi kujengwa upya. Hivyo tuzingatie misingi hii."
Wabunge wa Ujerumani nao walikasirishwa na hatua ya Vance ya kuzungumzia bila kutaja moja kwa moja mjadala wa ndani wa wagombea wa uchaguzi kabla ya uchaguzi wa mapema utakaofanyika Februari 23.
Vance alisema hakuna nafasi kya kuwazuia wengine akimaanisha hakuna nafasi ya vyama vikuu nchini humo kukataa kabisa kufanya kazi na chama kinachofuata siasa kali za mrengo wa kulia cha AfD.