Ujerumani: Mabadiliko ya Merz kukabiliwa na upinzani
1 Septemba 2025Mageuzi anayopanga kuyafanya Kansela Friedrich Merz hivi karibuni katika kodi na masuala ya ustawi yanaweza kuleta mzozo katika serikali yake ya muungano
Changamoto zinazoikabili serikali yake ni kubwa ikizingatiwa kuwa huu ni mwaka wa tatu kwa uchumi wa Ujerumani bila ukuaji wa pato la taifa. Hali ya ustawi na mfumo wa pensheni inashindwa kuendana na changamoto za idadi ya watu wakati bajeti ya serikali ya shirikisho ina upungufu wa dola bilioni 200 kwa mwaka 2027 hadi 2029
Mbali na ukubwa wa shughuli ya kufanya mageuzi, mabadiliko anayotaka kuyafanya Merz yanatarajiwa kukabiliwa na upinzanikutoka chama cha Social Democratic ingawa ana nia ya kuepusha mvutano kwenye serikali yake. Kansela Merz anafahamu kuwa kila mpasuko kama ule uliomhusu Jaji wa mahakama kuu mwanzoni mwa majira ya joto unaifanya serikali yake kuwa kama ile iliyosambaratika mwaka uliopita kabla ya muhula wake kwisha ya mtangulizi wake Olaf Scholz wa chama cha SPD.
Mtaalamu wa Sayansi ya Jamii wa Chuo Kikuu cha Bochum Oliver Lembcke, anasema mtihani mkubwa wa Merz ni kati ya kukiridhisha chama chake au kuudumisha ushirika wake na SPD na hilo, si tatizo linaloweza kutatulika kwa urahisi.
Hii ni kwasababu Chama cha Merz cha CDU kilishafutillia mbali uwezekano wa kushirikiana na chama cha upinzani kisichotaka wageni cha Alternative for Germany AfD. Hivyo, chama cha Waziri wa Fedha na Naibu Kansela Lars Klingbeil cha SPDndicho kinachoshikilia kura ya turufu kwa Merz na chama chake cha CDU.
Changamoto kubwa ni katika suala la bajeti
Katika suala gumu la bajeti, Merz na Klingbeil watakuwa na matarajio kuwa kwa kongeza bajeti katika baadhi ya maeneo na kuzipunguza kwenye maeneo mengine na labda kwa kuongeza umri wa watu kustaafu, serikali itaweza kusawazisha hali bila kuyakera makundi mengi tofauti tofauti.
Merz anasisitiza kuwa mfumo wa sasa wa ustawi hauwezi tena kufadhiliwa lakini tayari ameshafanya makubaliano na chama ndugu cha Bavaria cha Christian Social Union (CSU) ambayo itaigharimu zaidi fedha serikali
Kwa upande wa SPD, chenyewe kiko katika wakati mgumu zaidi ya CDU kutokana na kura ya maoni inayokipa chama hicho asilimia 15 ya uungwaji mkono, baada ya kupata matokeo mabaya zaidi kwenye uchaguzi wa kitaifa uliopita uliofanyika Februari. Kwa maana hiyo, Katika mkutano wa chama chake hivi karibuni, Merz alisisitiza kuwa kupata maelewano katika suala zima la kufanikisha mageuzi anayokusudia kuyafanya kunakihusu chama chake na washirika SPD.
Haya yanajiri wakati uchaguzi wa serikali za mitaa ukitarajiwa kufanyika Septemba 14 mwaka huu karika Jimbo la North Rhein Westphalia. Uchaguzi huo unaotafsiriwa kama mtihani wa kwanza wa uchaguzi kwa serikali ya Merz, unaweza kushuhudia mabadiliko mengine katika uungwaji mkono wa chama chake ikiwemo pia uwezekano wa kuporomoka zaidi
Pamoja na hayo yote, mtaalamu wa Sayansi ya Siasa Ursula Münch anasema wanachama wa vyama vyote vinavyounda serikali havina budi kutambua kuwa viko katika muungano dhaifu. Chama cha CDU hakina nguvu na SPD ni dhaifu zaidi. Kwa maana hiyo vinahitaji kufahamu kuwa haviwezi kufanikiwa kwa kuwa na matakwa yasiyoleta maelewano. Münch anaongeza kuwa kwa upande wa umma wa Wajerumani, wapende wasipende maelewano ndiyo jambo pekee litakalosaidia, hata kama hayatomridhisha yeyote.