Meli za kijeshi za Marekani zavuka mlango bahari wa Taiwan
12 Februari 2025Meli mbili za kijeshi za Marekani zimeripotiwa kuvuka mlango bahari wa Taiwan mnamo wiki hii katika safari ya kwanza tangu Rais Donald Trump aingie madarakani mwezi uliopita, kitendo kilichoikasirisha China.
Soma: China yaapa kuyaangamiza kabisa majaribio yoyote ya uhuru wa Taiwan
Jeshi la China limesema meli hizo mbili za Marekani, ambazo limezitaja kuwa moja ni ya maangamizi na nyingine ya uchunguzi, zilivuka njia hiyo kati ya Jumatatu na Jumatano wiki hii na kuongeza kuwa vikosi vya China tayari vimetumwa ili kufuatilia.
Katika taarifa yake mapema leo Jumatano, kamandi ya mashariki ya jeshi la China, imesema kuwa hatua hiyo ya Marekani inatuma ishara mbaya na kuongeza hatari za kiusalama. Jeshi la Marekani pia limethibitisha meli zake kuvuka mlango bahari wa Taiwan ikisema ni utaratibu wa kawaida licha ya kuigadhabisha China.