Mashambulizi ya Israel nchini Yemen yauwa watu sita
25 Agosti 2025Msemaji wa Wizara ya Afya inayoendeshwa na Wahouthi amesema shambulizi la Israel liliwaua watu sita na kuwajeruhi 86. Mashambulizi hayo ndio ya karibuni kabisa katika zaidi ya mwaka mmoja wa mashambulizi ya moja kwa moja ya kisasi kati ya Israel na wanamgambo wa Houthi nchini Yemen, kwa sehemu kutokana na vita vinavyoendelea Gaza.
Wizara ya Ulinzi ya Israel ilichapisha picha Jumapili ikimuonesha Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu, Waziri wa Ulinzi Israel Katz na mkuu wa majeshi Eyal Zamir wakifuatilia mashambulizi hayo wakiwa kwenye handaki la kamandi ya kijeshi. Jeshi la Israel limesema lilishambulia eneo la kijeshi inakopatikana Ikulu, vituo viwili vya umeme na eneo la kuhifadhi mafuta.
Taarifa ya jeshi la Israel imesema mashambulizi hayo yalijibu mashambulizi ya mara kwa mara ya utawala wa kigaidi wa Wahouthi dhidi ya taifa la Israel na raia wake. Ijumaa iliyopita, Wahouthi walisema walirusha kombora kuelekea Israel kama hatua ya kuwaunga mkono Wapalestina kwenye Ukanda wa Gaza.