NATO NA EU kuipatia msaada zaidi wa kijeshi Ukraine
11 Aprili 2025Mawaziri wa ulinzi wa muungano wa mataifa yanayafahamika kama marafiki wa Ukraine,wamekubaliana leo, kuipatia msaada zaidi wa kijeshi nchi hiyo wa Yuro bilioni 21. Msaada huo umetangazwa katika mkutano wa mataifa hayo ulioongozwa kwa pamoja na Ujerumani na Uingereza, mjini Brussels.
Soma pia: Viongozi wa Ulaya waridhia kuongeza matumizi ya ulinziKatika mkutano huo uliofanyika kwenye makao makuu ya Jumuiya ya kujihami NATO mjini Brussels,waziri wa ulinzi wa Ujerumani Boris Pistorius alitowa mtazamo unaoonesha kwamba Urusi bado haina dhamira ya kufikia amani na Ukraine, na kufafanuwa kwamba nchi hiyo inahitaji kutambuwa kwamba Ukraine inaouwezo wa kuendelea na vita hivi.
"Kwa kutazama uchokozi unaoendelea kufanywa na Urusi dhidi ya Ukraine, tunapaswa kuondowa fikra kwamba amani nchini Ukraine inaweza kupatikana katika kipindi cha hivi karibuni. Tunapaswa kuhakikisha Ukraine inaendelea kupata msaada wetu wa pamoja wa kijeshi.Na Urusi inapaswa kuelewa kwamba Ukraine inaweza kuendelea na vita na tutaiunga mkono.''
Lakini pia waziri huyo wa ulinzi wa Ujerumani aliweka waziwazi kwenye mkutano huo wa Brussels kwamba nchi yake haiwezi kuipatia Ukraine mifumo mipya ya Ulinzi ya Patriot kwasababu, yenyewe Ujerumani inasubiri kuipata mifumo hiyo.
Soma pia: Wanachama wa NATO waahidi kuongeza matumizi yao ya ulinziMara kadhaa Ukraine imekuwa ikisisitiza kwamba inahitaji mifumo ya ulinzi wa anga yake hasa hasa hiyo ya Patriot kujilinda dhidi ya mashambulizi ya makombora yanayofanywa na Urusi. Mkutano huo wa mawaziri wa ulinzi wa Jumuiya ya NATO na Umoja wa Ulaya ambao ni kile kinachofahamika kama kundi la marafiki wa Ukraine, wameahidi msaada wa kijeshi wa yuro bilioni 21 kwa nchi hiyo. Rustem Umerov waziri wa ulinzi wa Ukraine alikuwa na ujumbe huu kwa mkutano huo.
"Tunashukuru kwa juhudi za muungano huu zilizooneshwa leo na kwa nchi zilizotowa mchango ambao ni miongoni mwa misaada mikubwa zaidi tuliyopata. Kama tulivyosikia leo ahadi iliyotolewa ni yuro bilioni 21 ni kiwango kikubwa,tunashukuru. Rais Volodymyr Zelensky anaomba tutazame ulinzi wa anga, tupate mifumo mipya ya ulinzi ya Patriot. Tumeshatowa ombi hili kwa washirika wetu na tunafanya kazi pamoja kupata mifumo hiyo''
Mkutano huo wa Brussels unafanyika chini ya kiwingu cha juhudi zinazofanywa na Marekani za kujaribu kuishinikiza Urusi na Ukraine kufikia makubaliano ya kusitisha vita.
Mjumbe wa rais Donald Trump Steve Witkoff amekutana leo na mjumbe wa rais Vladmir Putin wa masuala ya uwekezaji Kirrill Dmitriev, mjini St Petersburg, huku pia ripoti kutoka ikulu ya Kremlin zikionesha kwamba Wittkoff aatakutana na rais Putin baadae leo.