Makamu wa Rais wa Marekani Vance kukutana na Rais Zelensky
14 Februari 2025Makamu wa Rais wa Marekani J.D Vance anakutana Ijumaa na viongozi wa ulimwengu pamoja na wanadiplomasia wanaokusanyika mjini Munich, Ujerumani kwa ajili ya Mkutano wa Usalama katikati ya wasiwasi mkubwa na sintofahamu inayoibuliwa na sera ya kigeni ya Rais Donald Trump.
Mustakabali kuhusu Ukraine ni ajenda kubwa kwenye mkutano huo, baada ya mawasiliano ya simu kati ya Rais Trump na Rais wa Urusi Vladimir Putin mapema wiki hii, ambapo walikubaliana kushirikiana kuumaliza mzozo kati ya Urusi na Ukraine uliodumu kwa miaka mitatu.
Soma pia: Viongozi wa dunia wanakutana Munich kujadili usalama
Vance anatarajiwa kukutana na Rais Volodymyr Zelenskyy wa Ukraine baadae leo kwa mazungumzo ambayo wengi, na hasa Ulaya wanatumaini yataleta mwanga kuhusu mapendekezo ya Trump kuelekea suluhu ya vita hivyo.
Kwenye mahojiano yaliyochapishwa leo na Jarida la Wall Street, Vance ametishia kuiwekea Urusi vikwazo zaidi na pengine kuchukua hatua za kijeshi, ikiwa haitakubaliana na makubaliano ya kudumu ya amani.