Maelfu waandamana Mexico kuwakumbuka waliopotea
16 Machi 2025Maelfu ya watu nchini Mexico wameingia barabarani kushiriki mkesha wa nchi nzima kwa ajili ya watu wengi waliopotea. Waandamanaji katika miji kote nchini humo waliweka jozi 400 za viatu na mishumaa 400 chini kama ishara ya kumbukumbu ya watu ambao hadi sasa haijulikani walipo.
Maelfu ya watu hao wameonekana wakiwa wamebeba mabango yaliyoandikwa ''Mexico ni kaburi la watu wengi na sisi tunataka majibu''. Katika mji mkuu Mexico City, maandamano yamefanyika mbele ya Ikulu ya Kitaifa na katika makazi rasmi ya Rais Claudia Sheinbaum.
Soma zaidi.Trump aamuru kufungwa kwa muda kituo cha habari cha VOA
Kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini Mexico, maandamano hayo yanafanyika pia katika miji ya Guadalajara, Puebla, Veracruz, Cancún na Colima. Duru zinaeleza kwamba zaidi ya watu 124,000 wameorodheshwa rasmi kupotea kusikojulikana nchini Mexico, huku idadi kubwa ikihusishwa na biashara haramu ya ulanguzi wa dawa za kulevya.