Lebanon kujadili mpango wa kuipokonya silaha Hezbollah
5 Septemba 2025Mnamo mwezi Agosti, kutokana na shinikizo kubwa la Marekani na kwa hofu ya Israel kuongeza mashambulizi nchini humo, serikali ya Lebanon ililiamuru jeshi kuandaa mpango wa kulipokonya silaha kundi la Hizbullah kufikishia mwishoni mwa mwaka huu.
Hata hivyo, kundi hilo limepinga vikali mpango huo na kuutaja "usio wa kizalendo” na unaotumikia maslahi ya Marekani na Israel huku wabunge wake wakiitaka serikali kuufuta uamuzi huo wakionya kwamba unaweza kusababisha machafuko ya ndani.
Serikali imesema mpango huo ni sehemu ya makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyosimamiwa na Marekani mnamo mwezi Novemba na ambayo yalimaliza uhasama wa zaidi ya mwaka mmoja kati ya Hezbollah na Israel.
Kikao cha baraza la mawaziri cha kujadili mpango huo kimefanyika wakati mashambulizi ya anga ya Israel kusini mwa Lebanon yameongezeka katika muda wa siku mbili zilizopita na kusababisha vifo vya takribani watu watano.