Kiongozi wa kupambana na dawa za kulevya auawa Ecuador
15 Februari 2025Tukio hilo limetokea kwenye mji ulioathiriwa vibaya na uhalifu unaotokana na biashara hiyo haramu wa Guayaquil.
Polisi imesema Kanali Porfirio Cedeno, aliyekuwa kiongozi wa kikosi maalamu cha anga cha kupambana na mtandao wa wauza dawa za kulevya alipigwa risasi kadhaa wkati akiwa njiani kwenda kwenye hafla moja ya kijeshi.
Cedeno alikuwa anasafiri kutoka mji wa Guayaquil kwenda mji Manta, ambako ni umbali wa karibu saa tatu pale washambuliaji walipolimiminia gari lake risasi zaidi ya 20 na kumuua papo hapo.
Miji hiyo miwili imekuwa kitovu cha mapigano kati ya makundi hasimu ya ulanguzi wa dawa za kulevya na kuitumbukiza nchi hiyo Amerika ya Kusini kwenye machafuko.
Waziri wa Ulinzi wa Ecuador Gian Carlo Loffredo amesema mauaji ya Cedeno yanapaswa kujibiwa kwa vita kali dhidi ya magenge ya uhalifu.