Hezbollah yaionya Marekani kutoingilia utawala wa Lebanon
23 Februari 2025Kiongozi wa kundi la Hezbollah Naim Qassem amesema hawatokubali udhibiti na ushawishi wa Marekani kwa utawala mpya wa Lebanon unaoonekana kuwa karibu na nchi za Magharibi. Utawala huo uliibuka baada ya kundi hilo linaloungwa mkono na Iran na lililokuwa na usemi kwenye siasa za Lebanon kudhoofika kutokana na vita kati yake na Israel.
Qassem ameyasema hayo hii leo wakati wa hotuba yake iliyorushwa kwa njia ya Televisheni kwa maelfu ya waombolezaji waliohudhuria mazishi ya aliyekuwa kiongozi wa Hezbollah aliyeuawa Hassan Nasrallah mjini Beirut.
Qassem amesisitiza kuwa kundi hilo la wanamgambo limesalia imara na liko tayari kukabiliana na Israel licha ya mapatano ya mwezi Novemba kati ya Hezbollah na Israel.
Mapema mwezi huu, naibu mjumbe maalum wa Marekani kanda ya Mashariki ya Kati Morgan Ortagus alisema kundi hilo lilishindwa na Israel, na kutangaza mwisho wa utawala wa ugaidi wa Hezbollah.