Jeshi la Sudan lafanikiwa kudhibiti benki kuu ya nchi hiyo
22 Machi 2025Vikosi vya jeshi la Sudan vimechukua udhibiti wa makao makuu ya benki kuu ya nchi hiyo ikiwa ni mwendelezo wa mafanikio makubwa ya vikosi hivyo katika mji mkuu Khartoum dhidi ya wapiganaji wa kundi la wanamgambo wa (RSF). Taarifa hizo zimetolewa na vyanzo vya jeshi hilo kwa shirika la habari la Reuters hii leo Jumamosi.
Soma zaidi: Mataifa ya Ulaya: Mpango wa kusitisha vita gaza urejeshwe
Udhibiti huo unakuja siku moja baada ya kufanikiwa kurejesha udhibiti kamili wa ikulu ya rais baada ya miaka miwili. Mapema leo mkuu wa jeshi la Sudan Abdel Fattah al-Burhan alisema kwamba hakutakuwa na mazungumzo na vikosi vya RSF hadi watakapoachana na azma yao na kuweka silaha chini, huku akisisitiza kwamba mapambano yataendelea hadi watakapofanikiwa kulitokomeza kabisa kundi hilo.
Eneo la katikati mwa mji mkuu wa Sudan, Khartoum limekuwa kitovu cha mapigano makali kati ya pande hizo hasimu katika kipindi cha miezi ya karibuni.